Idadi ya wakimbizi wa ndani Ukraine yazidi kuongezeka

March 23, 2022 5:46 am · Herimina
Share
Tweet
Copy Link
  • Hadi Machi  16 wafikia milioni 6.5
  • Shirika la Umoja wa Mataifa la Uhamiaji laongeza misaada mbalimbali kwa wakimbizi hao
  • Ubaguzi wa rangi wawakumba wanaokimbilia nchi nyingine.

Dar es Salaam. Shirika la Umoja wa Mataifa la Uhamiaji (IOM) limesema kuwa mashambulizi yanayoendelea nchini Ukraine kwa takriban mwezi mmoja sasa yamesababisha zaidi ya watu milioni 6.48 kuwa wakimbizi wa ndani nchini humo. 

IOM imesema hayo Machi 21 jijini Geneva uswisi baaada ya kufanya utafiti katika wiki ya Machi 9 hadi 16, 2022. 

Utafiti huo unaonesha kuwa asilimia 13.5 ya wakimbizi hao wa ndani walishawahi kukumbwa na hali hiyo ya kukimbia makazi yao mwaka 2014 na 2015. 

IOM inabainisha kuwa wakimbizi wengi ni watu wenye mahitaji maalum ikiwemo wanawake wajawazito na wanaonyonyesha, wazee,  watu wenye magonjwa sugu na watu wenye ulemavu. 

“Timu zetu zimekuwa zikiwafikia maelfu ya watu na kuwapa misaada muhimu, lakini tunahitaji uhasama ukome ili kuweza kuwafikia watu katika maeneo yaliyoathirika zaidi,” anasema Mkurugenzi Mkuu wa IOM, António Vitorino.

Vitorino anasema kuwa kiwango cha mateso wanachopitia watu hao kinapita aina yoyote ya maswahibu mtu anayoweza kufikiri yanaweza kumtokea na kwamba kwa sasa kipaumbele cha shirika hilo ni kuwafikishia mahitaji wananchi waliokwama ndani ya nchi hiyo. 

IOM pia imeweka namba za simu za dharura kwenye kila kanda ili kusaidia wananchi wanaokimbia mapigano dhidi ya Urusi.

Kwa kushirikiana na ofisi inayoshughulikia wakimbizi wa ndani Ukraine, IOM imetoa msaada wa chakula na vyombo vya jikoni katika maeneo mawili ya makazi ya wakimbizi huko Zakarpattia na kutoa vifaa vya usafi katika taasisi nne za kijamii huko Luhansk. 

Hadi sasa, IOM imesambaza zaidi ya mablanketi 18,000 ya joto na vifaa vya usafi 8,000 kwa wakimbizi wa ndani walioko  katika mikoa ya Lviv, Ivano Frankivsk, Dnipro, Mykolaiv na Zakarpattia. 


Zinazohusiana:


Ubaguzi wa rangi nao umo

Wakati wakimbizi wa ndani nchini humo wakiendelea kupewa ahueni, hali imekuwa mbaya kwa wakimbizi wanaokimbilia nchi za jirani ambao inadaiwa wanabaguliwa.

Kamishna Mkuu wa shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi (UNHCR),  Filippo Grandi amesema ingawa ameguswa na uungwaji mkono unaoonekana kutoka kwa jamii zinazowakaribisha zaidi wakimbizi wa Ukraine tangu mashambulio kutoka Urusi yaanze, kuna wakimbizi wanapitia hali ya ubaguzi.

 “Tulishuhudia hali mbaya, kwamba baadhi ya watu weusi na kahawia wanaokimbia Ukraine na vita vingine na migogoro duniani kote  hawajapata kutendewa sawa na wakimbizi wa Ukraine,” amesema Grandi.

Grandi ameeleza hayo katika siku ya kimataifa ya kutokomeza ubaguzi wa rangi Machi 21 na kuongeza kuwa ni lazima kuongeza mshikamano na kulaani kwa uthabiti vitendo vya ubaguzi na upendeleo.

“Tunahitaji kuhakikisha kwamba ugawanaji wa uwajibikaji wa kimataifa unaimarishwa kwa wakimbizi wote, bila kujali wanatoka wapi,” amesisitiza Grandi.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW