Hapana: Somalia haijaikopesha Tanzania Sh972 bilioni
- Waziri wa Wizara ya Fedha na Mipango amewataka watanzania kupuuzia taarifa hiyo
- Kwa mujibu wa Wizara hiyo ni Sh978.6 bilioni zilizoahidiwa kukopesha nchini na Umoja wa Falme za Kiarabu (UEA)
Dar es Salaam. Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Mwigulu Nchemba amewataka Watanzania kupuuzia taarifa zinazosambaa mtandaoni kuwa Wizara yake imepokea mkopo wa Sh972 bilioni kutoka Somalia.
“Puuzieni upotoshaji, habari ya mwisho ndio sahihi,” amesema Nchemba kupitia ukurasa wake wa Instagram.
Kwa mujibu wa Wizara ya Fedha na Mipango, mkopo ambao Tanzania imeahidiwa kupewa ni Sh978.6 bilioni kutoka Mfuko wa Umoja wa Falme za Kiarabu na sio kutoka Somalia kama taarifa zinaazosambaa mtandaoni.
Fedha hizo zitatumika kutekeleza miradi mbalimbali ikiwemo mradi wa umeme wa Benaco-Kyaka mkoani Kagera na ujenzi wa makazi ya watumishi ya gharama nafuu visiwani Zanzibar.
Septemba 26, 2022 Waziri Nchemba alifanya ziara ya kikazi mjini Dubai kwenye Falme za Kiarabu (UEA) ambapo mbali na kuahidiwa mkopo huo alisaini mikataba mbalimbali ikiwemo mkataba wa makubaliano ya kuondoa utozaji kodi mara mbili na kuzuia ukwepaji wa kodi ya mapato, kati ya Tanzania na Umoja wa Falme za nchi za Kiarabu.
Soma zaidi
-
Mfumuko wa bei ya bidhaa wang’ang’ania kiwango cha Oktoba
-
Mapato mauzo nje ya nchi yapaa, dhahabu ikishuka kwa asilimia 1.1
Tulichobaini
Huenda taarifa hiyo ya uzushi ikawa imetengenezwa na watu wenye nia ya upotoshaji na siyo chombo cha habari cha Swahili Times kama inavyoonekana.
Utafiti uliofanywa na timu ya Nukta Fakti umebaini kuwa habari hiyo imehaririwa.
Kwa kutumia zana ya kigitali ya InVID inayotumika kuthibitisha habari kwa picha au video, tumebaini kuwa sehemu ya nyuma ya maandishi hayo imefutwa kwa wino mwekundu ili ifanane na nakala halisi ya chombo hicho cha habari.
Aina ya mwandiko iliyotumika kwenye taarifa hiyo haifanani kabisa na mwandiko halisi unaotumika na Swahili Times kwenye habari zao zinazoweka kwenye mitandao yao ya kijamii.
Sambamba na hayo habari hiyo haipo kwenye kurasa rasmi za mitandao ya kijamii zinazotumika na chombo hicho cha habari jambo linaloashiria huenda habari hiyo ni ya kughushi.
Kwenye ukurasa rasmi wa Instagram wa Swahili Times wameweka habari sahihi kuhusu Abu Dhabi kuikopesha Tanzania Sh978 bilioni tofauti na habari yauzushi inayosambaa.
Latest
