Deni la Serikali laongezeka kwa Sh8 trilioni ndani ya mwaka mmoja
- Ongezo la deni hilo limetokana na kupokelewa kwa mikopo mipya kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo.
- Tathmini zinasema deni la Serikali bado ni himilivu.
Dar es Salaam. Deni la Serikali limeongezeka kwa zaidi ya Sh8 trilioni ndani ya mwaka mmoja likichochewa na kupokelewa kwa mikopo mipya kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo.
Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Mwigulu Nchemba ameliambia Bunge leo kuwa deni hilo la Serikali lilifikia Sh69.44 trilioni Aprili 2022 kutoka na Sh60.72 trilioni kipindi kama hicho mwaka 2021 ikiwa ni sawa na ongezeko la asilimia 14.4.
Kwa hesabu hizo, deni la Serikali liliongezeka kwa Sh8.72 trilioni ndani ya mwaka mmoja.
“Kati ya kiasi hicho, deni la nje lilikuwa shilingi trilioni 47.07 na deni la ndani lilikuwa Sh22.37 trilioni,” amesema Dk Nchemba wakati akiwalisha Bungeni taarifa ya hali ya uchumi wa taifa kwa mwaka 2021 na mpango wa maendeleo wa taifa kwa mwaka 2022/2023
Ongezeko la deni hilo, amesema lilitokana na kupokelewa kwa mikopo mipya kutoka vyanzo vyenye masharti nafuu na ya kibiashara kwa ajili ya kugharamia miradi ya maendeleo.
“Aidha, ongezeko la deni limetokana na kutolewa kwa hatifungani maalumu yenye thamani ya Sh2.18 trilioni kwa ajili ya deni la Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) lililotokana na michango ya watumishi wa kabla ya mwaka 1999,” amesema Dk Nchemba.
Licha ya ongezeko la deni hilo, waziri huyo amesema taarifa ya tathmini ya uhimilivu wa deni iliyofanyika Novemba 2021 inaonesha kuwa deni la Serikali bado ni himilivu katika kipindi cha muda mfupi, wa kati na mrefu kwa kuzingatia ukomo wa viashiria vyote vinavyokubalika kimataifa.
Hata hivyo, kumekuwa na msukumo mkubwa miongoni mwa wadau wa maendeleo ambao wamekuwa wakionya juu ya kasi ya ongezeko la deni la Serikali ndani ya miaka mitano iliyopita.
Latest