Marekani yatafakari namna ya kutoa Sh3 trilioni kwa Tanzania

March 26, 2022 7:44 am · Mwandishi
Share
Tweet
Copy Link
  • Ni baada ya kupokea ombi la Tanzania ili izielekeze fedha hizo katika miradi ya kipaumbele.
  • Marekani imepanga kutoa fedha hizo kwa asasi za kiraia.

Dar es Salaam. Serikali ya Tanzania imeliomba Shirika la Maendeleo ya Kimataifa la Marekani (USAID) kuzielekezwa zaidi ya Sh3 trilioni katika miradi ya kipaumbele badala ya kuzipatia asasi za kiraia za Tanzania moja kwa moja.

USAID imepanga kutoa fedha hizo kwa asasi za kiraia katika kipindi cha miaka mitano ijayo ili kuimarisha utendaji na utekelezaji wa shughuli za kuwasaidia na kuboresha maisha ya wananchi. 

Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Mwigulu Nchemba ametoa maombi hayo Machi 25, 2022 mkoani Dodoma, alipofanya mazungumzo kwa njia ya mtandao na Mkurugenzi wa USAID, Kate Samvongsiri.

Dk Nchemba amesema ni kweli fedha hizo zina umuhimu katika miradi iliyokusudiwa kutekelezwa na asasi za kiraia lakini zielekezwe katika atika vipaumbele vya Samia Suluhu Hassan ikiwemo sekta za afya, elimu, kilimo, na zitakazochochea ukuaji wa uchumi.

“Tunapoandaa ushirikiano mpya na mipango mipya tunaomba mzingatie vipaumbele vya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan ambayo amewekeza nguvu kubwa, sambamba na yale mnayofanya kwenye sekta ya afya, elimu, kilimo, mazingira, pamoja na sekta zingine,” amesema Dk Mwigulu.

Amesema kwa sasa Rais Samia anajenga anatekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo na ameiomba USAID kuelekeza fedha hizo ambazo zinapitia kwenye mashirika yasiyo ya kiserikali (NGOs), katika maeneo hayo.

 “Mfano, vituo vya afya vingi vimejengwa na watumishi wataajiriwa, mnaweza mkaweka nguvu kwenye vitendea kazi ambavyo bado havijakamilika ili huduma ziwe zinapatikana na lengo la Serikali pamoja na malengo mliyonayo ya kuendeleza huduma za jamii ambalo mnalo liweze kutimia,” amesema Mwigulu.

Tanzania na USAID zimekuwa na uhusiano wa zaidi ya miaka 50, na mwaka 2016, shirika hilo lilisaini mikataba mitatu ya msaada yenye thamani za zaidi ya Dola za Marekani milioni 635.5 (Sh1.5 trilioni), zilizotumika kutekeleza miradi mbalimbali ya kiuchumi na kijamii, programu ambayo itafikia tamati mwezi Septemba, 2022.

Mkurugenzi wa USAID, Kate Samvongsiri, amesema kuwa wanapenda kushirikiana na Serikali ya Tanzania na watakaa pamoja na kuangalia shughuli zinazofanyika katika sekta hizo za elimu, afya, kilimo, maji pamoja na zingine na kuona namna watakavyoziwezesha.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW