WHO: Chanjo ya Uviko-19 inaokoa maisha tusiidharau
- Wataalamu wasisitiza kupuuzia taarifa potofu kuhusu chanjo.
- Wasema chanjo imeepusha vifo kwa zaidi ya watu milioni 20 kwa mwaka mmoja tu.
Dar es Salaam.Shirika la Afya Duniani (WHO) limeendelea kusisitiza umuhimu wa kupata chanjo ya Uviko-19 ili kujikinga na maambukizi ya virusi hivyo na kuwataka watu wote kupuuzia taarifa potofu zinazoendelea kutolewa kuhusiana na chanjo hizo.
Hivi karibuni kumekuwepo na taarifa mbalimbali zinazokosoa ufanisi wa chanjo ya Uviko-19, zikielezea kuwa chanjo hizo hazina uwezo wa kuzuia virusi vya Corona na kuwa asilimia kubwa ya watu waliopoteza maisha ni waliochanja.
Taarifa hizo zimeenea maradufu baada ya kuenea kwa video inayoonyesha waandishi wa habari wakimhoji Mkurugenzi wa kampuni ya madawa ya Pfizer ya nchini Marekani, Albert Bourla kuhusu ufanisi wa chanjo ya Uviko-19 aina ya Pfizer ambapo hata hivyo hakujibu kitu chochote.
Miongoni mwa maswali ambayo waandishi wa habari walimuuliza ni pamoja na je ni lini alitambua chanjo yake haizuii maambukizi, kwanini alikaa kimya, na ni kiasi gani cha faida alitengeneza kutokana na kuuza chanjo?
Dk Kate O’brien ambaye ni Mkurugenzi wa Chanjo, Kinga na Baiolojia kutoka WHO amesema ufanisi wa chanjo katika mwaka wa kwanza tu wa janga umeweza kuepusha vifo kwa zaidi ya watu milioni 20 duniani.
Soma zaidi:
- Tanzania na Uviko-19: Maambukizi yaongezeka kwa asilimia 62
- Watanzania wahimizwa kujikinga dhidi ya magonjwa ya mfumo wa hewa
- Kraken: Kirusi kipya cha Uviko-19 kinachowatesa wanasayansi
Dk Kate amesisitiza kuwa jambo lolote linalowakuta watu waliopata chanjo ya Uviko-19 halipaswi kuhusishwa moja kwa moja na chanjo, huku akiwaonya watu kuepuka taarifa potofu na kujitahidi kupata taarifa muhimu kwenye vyanzo sahihi.
“Napenda kuwatahadharisha watu kuhusiana na hizi ripoti za mitandao ya kijamii, ambazo zinawahusisha watu waliochanja na athari hasi kwenye afya zao, ni muhimu sana kupata taarifa kwenye vyanzo sahihi,” amesema Dk Kate.
Msisitizo huu unatolewa na WHO wakati ambao dunia inakabiliwa na wimbi jipya la maambukizi ya Uviko-19 kutoka kwa kirusi kipya cha Kranken ambacho tayari kimesababisha zaidi ya vifo 59,000 nchini China kwa mwezi mmoja pekee.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Teknolojia ya Chanjo wa WHO, Dk Maria Van Kerkhove amesisitiza kuwa chanjo pekee haitoshi bali kupata dozi kamili ya huku akizitaka Serikali kuwapa kipaumbele watu ambao wapo hatarini zaidi kupoteza maisha kutokana ugonjwa huo.
Kwa mujibu wa WHO, jumla ya dozi bilioni 13.1 za chanjo ya Uviko-19 zimeshatolewa sehemu mbalimbali duniani ambapo watu bilioni 5.4 wameshapata dozi moja ya chanjo na watu bilioni 5 wamepata chanjo kamili hadi kufikia Januari 20, 2023.
Tanzania kwa sasa iko mbioni kuzindua dozi ya ziada ya chanjo ya Uviko-19 ‘booster’ ambayo itatolewa kwa hiari kwa wale wote watakaokuwa wanahitaji kujiongezea kinga ya mwili.
Kwa mujibu wa Waziri wa Afya Ummy Mwalimu mpaka sasa tayari chanjo imekwishatolewa kwa zaidi ya asilimia 86 kwa watu wenye sifa wakiwemo wenye umri wa zaidi ya miaka 18.
Tangazo: