CCM, ACT-Wazalendo walivyotegua kitendawili cha maridhiano Zanzibar
- Ni baada ya kukamilika wa mazungumzo ya miezi nane.
- Rais Samia, Othman wasema maridhiano yanatija kwa Taifa.
Dar es Salaam. Hatimaye Chama cha Mapinduzi (CCM) na ACT-Wazalendo vimesaini tamko la pamoja la maridhiano ya kisiasa visiwani Zanzibar, hatua inayolenga kuimarisha ushirikiano wa kisiasa visiwani humo.
Tamko hilo limesainiwa katika hafla iliyofanyika Ikulu ya Zanzibar leo Julai 9, 2026, ikishuhudiwa na Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk Hussein Mwinyi, pamoja na Mwenyekiti wa ACT-Wazalendo Taifa, Othman Masoud Othman.
Akizungumza katika hafla hiyo Rais Samia amesema tukio hilo linafungua ukurasa mpya wa amani na utulivu viswani Zanzibar na Tanzania kwa ujumla.
“Maridhiano si udhaifu bali ni ukomavu wa kisiasa unaojenga misingi ya umoja na kuheshimiana…Mwelekeo huu wa kiungwana tulio ushuhudia leo, unafungua ukurasa mwingine katika kuimarisha umoja, amani, utulivu na mshikamano wa wananchi,” amesema Rais Samia.
Naye Mwenyekiti wa ACT- Wazalendo Othman Masoud ameeleza kuwa maridhiano na mazungumzo ya kisiasa visiwani Zanzibar ni kwa manufaa ya nchi, akiwataka wananchi kuwapinga wanaoyabeza au kuyapinga.
Matumaini baada ya miezi 8
Safari ya mazungumzo ya maridhiano kati ya CCM na ACT-Wazalendo ilianza Novemba 9, 2025, siku chache baada ya sintofahamu ya kisiasa iliyojitokeza kufuatia Uchaguzi Mkuu wa Zanzibar.
Kwa kipindi cha miezi minane, viongozi wa vyama hivyo waliendesha mazungumzo yaliyolenga kujenga uaminifu, kurejesha ushirikiano wa kisiasa na kutafuta suluhu ya tofauti zilizojitokeza baada ya uchaguzi.
Kusainiwa kwa tamko hilo kunaashiria kufungwa kwa hatua ya mazungumzo na kufunguliwa kwa awamu mpya ya ushirikiano, huku wakitarajia kuunda chombo kmaalum kitakachosimamia utekelezaji wa makubaliano yaliyofikiwa.
Hatua hiyo iliyofikiwa leo inaendeleza ajenda ya R4 iliyoanzishwa na Rais Samia mwaka 2021, ikijumuisha kufanya maridhiano na vyama vya siasa vya upinzani, suala lililosaidia kupunguza mvutano wa kisiasa iliyokuwa ikiendelea wakati huo.
Wakati Taifa lilipoingia katika vurugu za wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025 Rais Samia alifungua tena ukurasa wa maridhiano baada ya kutangazwa mshindi wa nafasi ya urais kwa lengo la kuliponya Taifa na kurejesha ustawi wa vyama vya siasa nchini.
Hata hivyo, bado baadhi ya vyama vya siasa havijajiunga na mchakato wa maridhiano vikisisitiza kuwa hatua hiyo itatafikiwa iwapo Serikali itafanya baadhi ya mageuzi ya kisiasa, ikiwemo kuanza kwa mchakato wa Katiba mpya.