Canada yapiga marufuku matumizi ya mtandao wa Tiktok
- Ni kwa wafanyakazi wote wa Serikali.
- Ni baada ya Umoja wa Ulaya na Marekani kuchukua hatua kama hiyo.
- Hofu ya usalama wa data yatajwa kama sababu.
Dar es Salaam. Ukiwa umepita mwaka mmoja tangu Serikali ya Marekani iupige marufuku mtandao wa Tiktok nchini humo, Serikali ya Canada nayo imepiga marufuku matumizi ya mtandao huo kwa vifaa vyote vinavyomilikiwa na Serikali yake.
Marufuku hiyo pia imewalenga wafanyakazi wa Serikali ya nchi hiyo kutotumia mtandao huo katika simu zao binafsi.
Waziri Mkuu wa Canada Justin Trudeau amesema huenda kukawa au kusiwe na hatua zaidi zitakazochukuliwa na Serikali ya nchi yake na kuongeza kuwa hatua hiyo imetokana na uwepo wa wasiwasi kuhusu usalama wa data.
“Serikali inapowaambia wafanyakazi wake wasitumie tena mtandao wa TikTok kwenye simu zao za kazi, wengi watahusianisha na usalama wa data zao, tunawapa taarifa ili wafanye maamuzi sahihi kwa ajili yao,” amesema Trudeau.
Mtandao huo wa kubadilishana video unaomilikiwa na kampuni ya nchini China ya ByteDance, hivi karibuni umeandamwa na shutuma pamoja na uchunguzi unaofanywa na nchi za magharibi kutokana na hofu kwamba huenda taarifa za watumiaji wa mtandao huo zikachukuliwa na Serikali ya China.
Zinazohusiana
- Dhana tano potofu kuhusu matumizi ya friji nyumbani
- Makosa unayotakiwa kuepuka wakati unatumia simu yako
- Mbinu tano za kudhibiti matumizi makubwa ya intaneti kwenye ‘smartphones’
Taarifa kama majina, umri, uraia, pamoja na namba ya simu ni miongoni mwa data ambazo huchukuliwa na tovuti au mitandao ya kijamii wakati wa kujisajili ili kutumia mtandao husika.
Siku tano zilizopita Tume ya Umoja wa Ulaya (EU) nayo ilitangaza kupiga marufuku kwa wafanyakazi wa umoja huo kumiliki mtandao huo katika simu zao au katika vifaa vya mawasiliano vya ofisi hiyo.
Tangu kuanzishwa kwake mwaka 2017, TikTok umegeuka kuwa mtandao pendwa hususan na vijana ambao wamekuwa wakibuni maudhui mbalimbali kwa njia ya video ambapo hutumia kama njia mojawapo ya kujipatia kipato na burudani.
Kupitia mtandao huo watu kadhaa wamejizolea umaarufu nchini Tanzania kutokana na aina ya maudhui wanayochapisha akiwemo Mtanzania Killy Paul ambaye alipata fursa ya kwenda kutumbuiza kwenye tamasha la muziki nchini India kupitia mtandao huo.
Kwa mujibu wa Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC), mtandao wa Tiktok mwaka 2021 uliipiku watumiaji mtandao wa Google jambo ambalo halikuwahi kufanyika kwa miaka 10 iliyiopita.
Mpaka sasa mtandao huo umepakuliwa na watu zaidi ya bilioni 1 duniani kote na kuufanya kuwa mtandao uliopakuliwa zaidi ukifuatiwa na mtandao wa Instagram na Facebook.