Dk Mpango: Waliotajwa ripoti ya CAG ‘watakipata cha moto’
Makamu wa Rais Dk Philip Mpango aliyekuwa akizungumza leo Aprili 11, 2023 aliposimama kuwasalimia wananchi katika kijiji cha Hughumalwa wilayani Kwimba mkoani Mwanza amesema tayari Serikali imeanza kuwashughulikia waliokula fedha za wananchi ambao wameibuliwa kwenye ripoti ya CAG na kuwa wote waliohusika ‘watakipata cha moto.’ Picha | Mariam John.
- Asema Serikali itawachukulia hatua wote waliohusika na ubadhirifu.
- Awataka wananchi kusimamia miradi ya maendeleo isharibiwe.
Dar es Salaam. Makamu wa Rais Dk Philip Mpango amewataka viongozi wa Serikali kuhakikisha wanasimamia kikamilifu utekelezwaji wa miradi ya maendeleo katika maeneo yao ili kusipatikane madudu yanayoibuliwa na ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) ya mwaka 2021/22.
Ripoti ya CAG iliyowasilishwa bungeni wiki iliyopita imeibua mjadala mpana kwenye jamii baada ya kubainika kwa ufisadi katika baadhi ya taasisi za umma zikiwemo baadhi ya halmashauri na mashirika likiwemo Shirika la Reli Tanzania (TRC)
Moja ya mapendekezo ya CAG Charles ni kuundwa kwa tume huru ya kuchunguza matumizi mabaya ya ofisi ya Mwendesha Mashtaka wa Serikali (DPP) na kuchukuliwa hatua za kisheria kwa watu waliohusika na ubadhirifu wa fedha za umma.
Dk Mpango aliyekuwa akizungumza leo Aprili 11, 2023 aliposimama kuwasalimia wananchi katika kijiji cha Hughumalwa wilayani Kwimba mkoani Mwanza amesema tayari Serikali imeanza kuwashughulikia waliokula fedha za wananchi ambao wameibuliwa kwenye ripoti ya CAG na kuwa wote waliohusika ‘watakipata cha moto.’
“Naomba taarifa za CAG zisisikike hapa na Mkoa wa Mwanza kwa ujumla, viongozi wote wanaohusika na kusimamia miradi wasimamie vizuri fedha hizo na asiwepo wa kudokoa,” amesema Dk Mpango na kusema wote waliohusika na ubadhirifu wa fedha za umma watashughulikiwa kisheria.
Zinazohusiana:
-
Hasara ya ATCL yapungua, Rais Samia aanika madudu mapya
-
Ripoti ya CAG: ATCL ilipata hasara ya Sh60 bilioni 2019-20
Makamu huyo wa Rais pia amewataka wananchi kuhakikisha wanatunza miundombinu ya kutolea huduma za kijamii katika maeneo yao kwa kuwa fedha zinazotumika katika kutekeleza ni kodi zao.
” Hizi fedha zinazotekeleza miradi hii ya maendeleo ni kodi zenu nyinyi wananchi pia hata hizo tunazokopa huko. Hivyo niwaombe mtunze miundombinu hiyo ili iweze kutumika kama ilivyokusudiwa,” amesema Dk Mpango.
Amemwagiza Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Profesa Makame Mbarawa kuhakikisha anasimamia kikamilifu suala la ujenzi wa barabara ya kilomita 10 kutoka Isandula kwenda Gundu ili ikamilike ifikapo nusu ya pili ya bajeti katika mwaka ujao wa fedha.
Agizo hilo limetolewa baada ya wabunge wa jimbo la Sumve, Sangalali Mageni na yule wa Kwimba Shanif Mansoor kusema kuwa barabara hiyo ambayo ni sehemu ya kilomita 71 katika majimbo hayo mawili iliahidiwa kujengwa kwa kiwango cha lami katika ilani ya chama cha mapinduzi ya mwaka 2020-2025.
Kutokana na maombi hayo Makamu alimwagiza Meneja wa Tanroad mkoa wa Mwanza, Paschal Ambrose kuhakikisha anatekeleza ujenzi huo na ukamilike ifikapo nusu ya pili ya mwaka wa bajeti ujao.
Awali Menena huyo wa Tanroad alimwambia Mkamau wa rais kuwa tayari wamepokea kiasi cha Sh500 milioni na kwamba mkandarasi amepatikana na ameanza kutekeleza ujenzi wa mzunguko (Roundabout) katika kijiji cha Izidaba ambapo baada ya kukamilisha atajenga na mita 250 ya barabara.
Latest