Rais Mwinyi atoa maagizo 5 siku ya uhuru wa vyombo vya habari duniani
- Ni pamoja na kuitumia siku hii kuweka mkazo mkubwa katika uhuru wa kujieleza.
- Asema uhuru wa kujieleza unakua kwa kasi ya kuridhisha.
- Waziri aahidi kukamilisha mchakato wa sheria ya habari haraka iwezekanavyo.
Dar es Salaam. Rais wa Zanzibar Dk Hussein Mwinyi amesema siku ya uhuru wa vyombo vya habari duniani itumike kuimarisha tasnia ya habari kwa kufanya mambo matano muhimu ikiwemo kuweka mkazo katika uhuru wa kujieleza ndani ya ajenda ya jumla ya haki za binadamu.
Rais Mwinyi aliyekuwa akizungumza katika kilele cha maadhimisho ya miaka 30 ya uhuru wa vyombo vya habari leo Mei 3, 2023 visiwani Zanzibar amebainisha kuwa siku hiyo itumike pia kufanya hafla zinazoangazia uhusiano wa haki ya kujieleza na uhuru wa kujieleza pamoja na kushirikiana katika kulinda uhuru wa vyombo vya habari.
“Siku hii ishirikishe wahusika wote kwa madhumuni ya kulinda uhuru wa vyombo vya habari, kuimarisha uhuru wa kujieleza na kuweka mazingatio kwamba haki za binadamu ni kitovu cha kufanya maamuzi katika ngazi ya kimataifa kikanda na kitaifa,” amesema Rais Mwinyi.
Mwinyi ameongeza kuwa ili kufikia Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDG’s) kila nchi mwanachama wa Umoja wa Mataifa (UN) zitumie siku hii kutimiza ahadi zao pamoja na kuungana na mashirika ya kupigania masuala ya mazingira, haki za wanawake na watoto na vita dhidi ya ufisadi.
Miaka 30 ya #WPFD
“Napenda nipongeze jitihada za #VyomboVyaHabari katika kufichua vitendo viovu ambavyo katika vipindi vya nyuma vilikua haviripotiwi vitendo hivi ni pamoja na #UnyanyasajiWaKijinsia, mauaji ya vikongwe na albino”
Rais wa Zanzibar, Mhe. Dkt Hussein Ali Mwinyi pic.twitter.com/vCG1gD6O6m
— World Press Freedom Day Tanzania (@Wpfd_Tanzania) May 3, 2023
Uhuru wa vyombo vya habari umekua
Kwa mujibu wa Rais Mwinyi kutokana na Serikali ya Tanzania kutambua mchango wa vyombo vya habari, uhuru wa kujieleza na uhuru wa vyombo vya habari umeendelea kukua ili kutoa nafasi kwa vyombo hivyo kuisaidia Serikali katika masuala mbalimbali ikiwemo kuibua ufisadi na uvunjifu wa sheria.
“Taarifa zinaonesha mpaka Februari 2023, kulikuwa na jumla ya redio 218, Televisheni 68, redio za kimtandao nane, televisheni za mtandao 391, blogu na majukwaa 73, Cable operators 53, pamoja na magazeti 312 yaliyosajiliwa Tanzania bara,” amebainisha Rais Mwinyi.
Kwa upande wa Zanzibar kumekuwa na ongezeko kubwa la vyombo vya habari kati ya mwaka 2020 hadi 2023 ambapo mpaka sasa kuna jumla ya televisheni 21, televisheni za mtandao 38, pamoja na redio 27.
Rais mwinyi amewaambia wanahabari kuwa kukua kwa sayansi na teknolojia ndiko kumechangia ukuaji huo ambao umechochewa na mabadiliko ya sheria kwani ndizo zinaruhusu usajili wa vyombo hivyo.
Amesema wingi wa vyombo vya habari unachochea kasi ya usambazaji na uenezaji wa habari.
Zinazohusiana:
- LHRC yazungumzia adhabu ya vituo vitatu vya televisheni mtandaoni.
- Waziri Nape ayafungulia magazeti manne yaliyofungiwa
- CCM yazidi kuongeza umiliki wa vyombo vya habari Tanzania
Sheria ya habari imekamilika
Kama ilivyo kwa Tanzania Bara, visiwani Zanzibar nao wanasubiri Sheria ya Vyombo vya Habari ambapo Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo Zanzibar Tabia Maulid Mwita amesema sheria hiyo ipo tayari na itawasilishwa kwa Baraza la Mapinduzi hivi karibuni ili ijadiliwe.
“Takribani asilimia 80 ya mchakato wa kupata Sheria ya Vyombo vya Habari Zanzibar imekwisha kamilika, hatua zilizobaki ni chache sana nimewaomba subira, muswada ule utakwenda baraza la wawakilishi, nawahakikishia sheria ile imezingatia maoni yenu mliyotoa,” amesema Waziri Tabia.
Kila mwaka ifikapo Mei 3, ulimwengu huadhimisha siku ya uhuru wa vyombo vya habari ili kuenzi mchango wa tasnia hiyo kwa jamii ambapo kidunia yanafanyika nchini Marekani, Barani Afrika yanafanyika nchini Zambia na kwa hapa Tanzania yamefanyika visiwani Zanzibar.
Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Mhe. Tabia Maulid Mwita akifungua Kongamano la Miaka 30 ya Siku ya Uhuru wa Vyombo vya Habari Duniani ambalo limeanza leo Mei 01 hadi Mei 03, 2023 kwenye Ukumbi wa Hotel ya Golden Tulip, Zanzibar. Picha | Habari-MAELEZO.