Serikali yaanika ukweli mwanafunzi kubadilishiwa namba kidato cha nne
- Yasema mwanafunzi huyo aliwadanyanga wazazi, walezi.
- Waziri Mchengerwa aonya usazambaji wa taarifa zisizo sahihi.
Dar es Salaam. Serikali imetolea ufanunuzi taarifa iliyosambaa katika mitandao ya kijamii kuhusu mwanafunzi aliyedai kubadilishiwa namba ya mtihani wa kidato cha nne na kushindwa kujiunga na masomo ya kidato cha tano yaliyoanza mwezi Agosti mwaka huu.
Taarifa iliyotolewa na Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini Nteghenjwa Hoseah Septemba 25, 2023 inasema taarifa hizo ni za uongo zipuuzwe.
“Tunapenda kuujulisha umma kuwa hakuna mwanafunzi aliyenyang’anywa haki yake ya kuendelea na masomo ya kidato cha tano na taarifa zilizotolewa na binti huyo ni za uongo na zipuuzwe…,” imesema taarifa ya Hosseah.
Mijadala iliibuka katika mitandao ya kijamii siku kadhaa zilizopita mara baada ya kuanza kusambaa kwa taarifa ya mwanafunzi aliyefahamika kwa jina la Sifika Daniel Ruben kudai ameshindwa kuanza masomo ya kidato cha tano kutokana na nafasi yake kupewa mtu mwingine.
Soma zaidi : Hajatulia: Rais Samia amteua Maharage Chande kuwa Postamasta Mkuu
Mwanafunzi huyo alidai amehitimu kidato cha nne katika Shule ya Sekondari Mkombozi iliyopo Same mkoani Kilimanjaro na kupangiwa kidato cha tano shule ya Sekondari Namwai iliyopo mkoani humo.
Aidha mwanafunzi huyo alidai amechelewa kuripoti shuleni hapo kutokana na kukosa mahitaji muhimu kwa wakati hadi alipopata wafadhili.
Hata hivyo kwa mujibu wa Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi) mwanafunzi huyo aliwadanganya walezi wake na kughushi jina pamoja na matokeo yake ya kidato cha nne.
“Imebainika kuwa binti anayelalamika mitandoni anaitwa Sifaeli Tawel Elirehema na alisoma shule moja na Sifika Daniel Ruben…
…Hata hivyo binti huyo namba yake ya mtihani ilikuwa ni S.850/135 alipata Div IV: 34 (Zero) na alisoma masomo ya Sanaa ilihali Sifika Daniel Ruben namba yake ya mtihani ni S.850/136 alisoma masomo ya Sayansi na amepata Division 1:10,” imefafanua taarifa hiyo.
Soma zaidi : Rais Samia apangua vigogo TTCL, Tanesco, vilio vya umeme vikiendelea Tanzania
Aidha Waziri wa Tamisemi, Mohamed Mchengerwa amewataka wazazi, walezi na wanaharakati kutokusambaza taarifa ambazo hawajajiridhisha na usahihi wake ili kuepuka kuzua taharuki kwenye jamii.
Awali, Mkuu wa Shule ya Sekondari ya Mkombozi aliyejitambulisha kwa jina moja tu la Nyambwiro B.A alitoa taarifa iliyofafanua kwa undani suala hilo akibainisha kuwa madai ya mwanafunzi huyo ni ya uongo kutokana na kukosa viambatanisho muhimu kama muhtasari wa matokeo yake (result slip).
Mwanafunzi anayeanza masomo ya kidato cha tano hutakiwa kuwa na result slip ili kuthibitisha taarifa zake na hutolewa katika shule aliyomaliza kidato cha nne.
Latest