Mapya yaibuka mwanafunzi kubadilishiwa namba ya mtihani
- Serikali yakiri ni kweli Iptisum Slim na wenzake sita walibadilishiwa namba za mitihani.
- Shule waliyokuwa wakisoma ya Chalinze Modern Islamic Pre and Primary iliyoko mkoani Pwani yaungiwa kuwa kituo cha mtihani kwa muda usiojulikana.
- Watumishi waliohusika kuchukuliwa hatua kali za kisheria.
Dar es Salaam. Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda ameagiza Shule ya Chalinze Modern Islamic Pre and Primary iliyoko mkoani Pwani kufungiwa kuwa kituo cha mtihani kwa muda usiojulikana.
Hataua hiyo imekuja baada ya kubainika kuwa shule hiyo iliwabadilishia namba za mitihani wanafunzi saba katika mtihani wa darasa la saba uliofanyika Oktoba 5 na 6 mwaka huu.
Mmoja wa wanafunzi hao, Iptisum Slim siku chache zilizopita alimuomba Prof Mkenda kuingilia kati suala hilo la madai ya kufanya mtihani na namba isiyo ya kwake.
Iptisum kupitia video fupi iliyokuwa akisambaa mtandaoni alionekana akiomba msaada na kusema siku ya mtihani alivyoingia darasani alipangiwa namba 40 na wakati karatasi ya kusaini ilivyopita alisaini namba 39.
“Baada ya mtihani kuisha baadhi ya wanafunzi tuliitwa na mwalimu mkuu tukaambiwa yale yaliyotokea yasisikike sehemu nyingine yaishie palepale,” anaeleza Iptisum katika video hiyo.
Aliomba asaidiwe kisheria kupata haki yake na majibu yake yarudi kwenye namba yake kwa sababu mtoto aliyemfanyia mtihani anashika nafasi ya chini na yeye anashika nafasi za juu huku akieleza kuwa katika mtihani wa Moko wilaya alishika nafasi ya kwaza.
Profesa Mkenda amesema baada ya kufanyika uchunguzi wamebaini kuwa ni kweli mwanafunzi huyo pamoja na wanafunzi wengine sita walibadilishiwa namba ya mtihani katika mtihani wa taifa wa darasa la saba.
“Ulichosema ni kweli na kimethibitishwa. Ni kweli ulibadilishiwa namba (Iptisum). Kwa hiyo sasa utasahishiwa mtihani wako kwa namba halali uliyotakiwa kufanyia mtihani,” amesema Profesa Mkenda leo Jumanne Oktoba 25, 2022 akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es salaam.
Ameagiza watumishi waliohusika na udanganyifu katika mtihani wa darasa la saba Shule ya Chalinze Modern Islamic Pre and Primary kuchukuliwa hatua huku shule hiyo ikisimamishwa kwa muda usiojulikana kuwa kituo cha mitihani.
Latest