Ahueni: Mfumuko wa bei washuka baada ya kung’ang’ania kiwango kimoja kwa miezi mitatu Tanzania
- Wapungua kwa asilimia moja na kufikia 3.2.
- Kupungua kwa bei ya bidhaa za vyakula kwatajwa kama sababu.
- Kasi ya mfumuko wa bei yapungua Uganda na na kupaa nchini Kenya.
Dar es Salaam. Kasi ya mfumuko wa bei za bidhaa na huduma nchini Tanzania kwa mwaka unaoishia Oktoba 2023 imepungua kwa asilimia moja na kufikia asilimia 3.2 kutoka asilimia 3.3 iliyorekodiwa mwaka unaoishia Septemba mwaka huu.
Kasi hiyo ya mfumuko wa bei kwa mwaka unaoishia Oktoba 2023 imepungua baada kung’ang’ania kiwango kimoja kwa miezi mitatu mfululizo yaani asilimia 3.3.
Taarifa ya mwenendo wa mfumuko wa bei nchini iliyotolewa leo Novemba 8, 2023 na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) inasema hali hiyo imechangiwa zaidi na kupungua kwa bei ya bidhaa za chakula.
Soma zaidi : MV Logos Hope: maktaba inayoelea inavyohamasisha usomaji wa vitabu duniani
“Hii inamaanisha kuwa, kasi ya mabadiliko ya bei za bidhaa na huduma kwa mwaka ulioishia mwezi Oktoba, 2023 imepungua ikilinganishwa na kasi iliyokuwepo kwa mwaka ulioishia mwezi Septemba, 2023…
“….kupungua kwa mfumuko wa bei wa Taifa kwa mwaka ulioishia mwezi Oktoba, 2023 kumechangiwa na kupungua kwa mfumuko wa bei kwa baadhi ya bidhaa za chakula kwa kipindi cha mwaka ulioishia mwezi Oktoba…,” imesema taarifa hiyo.
Itakumbukwa kuwa kiwango cha kasi ya mfumuko wa bei cha 3.1 kilichoripotiwa kwa mwezi huu ndio kiwango kidogo zaidi kuwahi kurekodiwa tangu mwaka 2021.
Mara ya mwisho kasi ya mfumuko wa bei wa taifa wa asilimia 3.3 iliripotiwa katika mwaka ulioishia Aprili na Mei, 2021 na tangu wakati huo mfumuko wa bei ulikuwa ukipanda na kushuka lakini haukuwahi kushuka zaidi ya kiwango hicho.
Bidhaa zilizochangia kushuka kwa mfumuko wa bei
Baadhi ya bidhaa za vyakula zilizoonesha kupungua kwa mfumuko wa bei kwa mwaka ulioishia Oktoba 2023, ni pamoja na ngano, mchele, nyama, mayai, samaki wabichi, dagaa, ndizi za kupika, mafuta ya kupikia, na njegere.
Aidha, NBS imeeleza kuwa mfumuko wa bei wa bidhaa za vyakula na vinywaji baridi kwa mwaka ulioishia Oktoba, 2023 nao umepungua hadi asilimia 4.5 kutoka asilimia 5.6 uliyorekodiwa mwaka ulioishia Septemba, 2023.
Kwa upande wa mfumuko wa bei ambao haujumuishi bidhaa za vyakula na vinywaji baridi kwa Septemba, 2023 umeongezeka kidogo na kufikia asilimia 2.6 kutoka asilimia 2.4 iliyorekodiwa mwaka ulioishia Oktoba, 2023.
Soma zaidi : Faida, hasara za kupungua kwa wakulima Tanzania
Vilio, ahueni nchi jirani
Wakati mfumuko wa bei ukipungua kidogo nchini, nchi jirani zimepata ahueni na vilio mara baada ya viwango vya mfumuko wa bei kupanda na kushuka.
Nchini Kenya mfumuko wa bei kwa mwaka ulioishia Oktoba, 2023 umeongezeka hadi asilimia 6.9 kutoka asilimia 6.8. kwa mwaka ulioishia Septemba, 2023.
Wakati Kenya ikipata maumivu, walaji nchini Uganda wamepata ahueni mara baada ya mfumuko wa bei kushuka hadi asilimia 2.4 kutoka asilimia 2.7 mwaka ulioishia Oktoba, 2023.
Latest