Utafiti:Zaidi ya watanzania milioni sita hawatumii vyoo
- Asilimia 10 hawana vyoo katika maeneo wanayoishi.
- Mkoa wa Simiyu waongoza kwa kuwa idadi kubwa ya watu wasiokuwa na vyoo.
- Waziri Ummy atoa maagizo kupunguza idadi ya wasio na vyoo nchini.
Dar es Salaam. Licha ya umuhimu wa choo katika maisha ya binadamu, baadhi ya wakazi nchini hawana maeneo rasmi kwa ajili ya huduma hiyo jambo linalohatarisha usalama wa afya na mazingira yanayowazunguka.
Ripoti ya Utafiti wa Afya ya Uzazi na Mtoto na Viashiria vya Malaria Tanzania (THDS-MIS) kwa mwaka 2022 inaonyesha asilimia 10 ya watanzania wanajisaidia katika maeneo ya wazi kutokana na kukosa vyoo katika makazi yao.
“Kujisadia maeneo ya wazi kunafanywa na asilimia 10 ya watu katika kaya za Tanzania bara na asilimia 7 Zanzibar.Vitendo hivyo vinafanyika kulingana na utofauti wa maeneo,” imesema ripoti hiyo.
Kwa mujibu wa sensa ya watu wa makazi ya mwaka 2022 asilimia hizo ni sawa na kusema watanzania milioni 6.1 wanaishi bila kuwa kuwa na vyoo.
Kati ya idadi hiyo, wanaoishi vijijini ndio wanaoongoza kwa ukosefu wa vyoo kulinganisha na wale wanaoishi maeneo ya mijini.

Simiyu kinara wa uhaba wa vyoo
Mkoa wa simiyu wenye jumla ya wakazi milioni 2.1 umeongoza kwa kuwa na asilimia 24 ya watu wasiokuwa na vyoo.
Hiyo ni sawa na kusema wakazi 504, 000 mkoani humo hawana huduma ya choo katika maeneo yao ya makazi.
Mbali na Simiyu mikoa mingine yenye idadi kubwa ya watu wasiokuwa na vyoo ni pamoja na Manyara asilimia 23, Tabora ( asilimia 22) Arusha na Mara asilimia 21.
Hata hivyo, matumizi ya vyoo kitaifa yameongezeka kwa asilimia 54 ndani ya miaka 6 jambo linaloendelea kutoa matumaini ya kuimarika kwa upatikanaji wa huduma hiyo nchini.
Mwaka 2015-2016 nchini Tanzania kulikuwa na asilimia 21 za matumizi ya huduma bora za choo iliyoongezeka hadi kufikia 75 katika utafiti uliofanyika mwaka 2022.
Miongoni mwa mikoa yenye matumizi bora ya vyoo pamoja mkoa wa Dar es Salaam ambao asilimia 99 ya wakazi wake wanapata huduma bora za choo, ikifuatiwa na mkoa wa Ruvuma wenye asilimia 92.
Soma zaidi:‘Betting’, vinywaji baridi kuchangia bima ya afya kwa wote Tanzania
Waziri Ummy atoa maagizo kudhibiti uhaba wa vyoo
Waziri wa afya, Ummy Mwalimu aliyekuwa akizungumza wakati wa maadhimisho ya siku ya choo duniani yaliyofanyika Novemba 19, 2023 jijini Tanga ametoa maagizo kwa wakuu wa mikoa na halmashauri kuendeleza jitihada za kupambana na uhaba wa vyoo katika maeneo yao.
“Katika kuendelea kuwezesha jamii kujenga na kutumia vyoo bora, naielekeza mikoa na halmashauri kutekeleza mambo yafuatayo…kufanya ukaguzi kwenye kaya, sehemu za Jumuiya, maeneo ya biashara na taasisi zote kwa kuhakikisha zinajenga na kutumia vyoo bora” amesema Waziri Ummy.
Maagizo mengine aliyoyatoa kiongozi huyo ni pamoja na kusimamia matumizi ya vyoo kwa wasafiri ikiwemo kutenge maeneo maalum kwa wasafiri kupata huduma hizo na kusimamia sheria za afya ya jamii zinazohusiana na ujenzi na matumizi ya choo bora kwenye ngazi ya kaya, taasisi na maeneo ya Jumuiya.