Malalamiko kupanda gharama za maisha yaongezeka

August 26, 2022 12:00 pm · Lucy Samson
Share
Tweet
Copy Link
  • Zatajwa kama changamoto kuu zinazowakabili Watanzania.
  • Wapendekeza Rais azipe kipaumbele.

Dar es Salaam. Utafiti mpya uliotolewa na taasisi ya Twaweza umeeleza kuwa takriban nusu ya Watanzania wanalalamikia kupanda kwa gharama za maisha kama moja ya changamoto kubwa inayozikabili katika kaya zao, huku wakitaka changamoto hiyo ipewe kipaumbele na Rais wakati wa kutafutiwa utatuzi.

Kwa kipindi cha zaidi ya miaka mitatu Watanzania wameshuhudia kuporomoka kwa uchumi na kupanda kwa gharama za maisha huku viongozi wa Serikali wakieleza kuwa athari za  janga la Uviko-19 pamoja vita ya Ukraine na Urusi vikichangia hali hiyo.

Ripoti ya utafiti uliofanywa na Twaweza kati ya Juni na Julai 2022 uliolenga kukusanya  maoni ya wananchi kuhusu hali ya uchumi wa Taifa, na tozo za miamala ya fedha kupitia simu za mkononi inaeleza kuwa wananchi 1,440 (asilimia 48) walioshiriki katika utafiti huo wametaja kupanda kwa gharama za maisha kama tatizo kubwa linalowakabili.

Hiyo ni sawa na kusema takriban watu 5 kati ya 10 wanalalamikia ugumu wa maisha kama changamoto inayowakabili kwa sasa.

Utafiti huo uliwashirikisha wahojiwa 3,000 kutoka awamu ya sita (Oktoba na Novemba 2021) na ya saba (Juni na Julai 2022) ya jopo maalum la Sauti za Wananchi. 

Changamoto nyingine zinazowakabili Watanzania ni ukosefu wa ajira na fursa nyingine za kujiingizia kipato kwa asilimia 29 pamoja na tatizo la njaa na uhaba wa chakula kwa asilimia 26 likiwakabili zaidi wakazi wa vijijini.

Hali ni mbaya zaidi kwa wakazi wa jiji la Dar es Salaam ambapo katika ripoti hiyo, asilimia 46 ya waliohojiwa wametaja kupanda kwa gharama za maisha kama changamoto kuu kwao.

Miji mingine, asilimia 44 wametaja gharama za maisha zipo juu huku vijijini ni asilimia 45.

Mbali na matatizo ya kiuchumi, matatizo ya huduma za kijamii yameongezeka kwa mwaka 2022 ukilinganisha miaka mingine  hususani kwenye vituo vya afya (asilimia 23), upatikanaji wa maji safi (asilimia 20), huduma za usafiri (asilimia 17) na elimu elimu kwa asilimia 15. 

“Kwa kipindi cha mwaka mmoja matatizo ya uhaba wa maji safi na salama yameongezeka kwa asilimia tisa  kutoka asilimia 11 mpaka asilimia 20 iliyofikiwa mwaka huu, hali ni mbaya zaidi kwenye tatizo la huduma duni za usafiri lililoongezeka kwa asilimia 10 na elimu kwa asilimia saba,” imeeleza sehemu ya ripoti hiyo.

Rukia Masayanyika, mshiriki wa masuala ya kijamii anasema wananchi wakishirikishwa katika masuala yanayohusu nchi yao ikiwemo tozo inaweza kusaidia kupunguza malalamiko ya mabadiliko hayo.


Soma zaidi:


Suluhu ya changamoto?

Wananchi walioshiriki utafiti huo wameeleza kuwa wakati Rais akipanga mipango yake ya kutatua changamoto za kijamii, wanafikiri suala la kupanda kwa gharama za maisha lipewe kipaumbele. 

Asilimia 46 ya waliohojiwa  wametaja gharama kubwa za maisha kuwa ni miongoni mwa masuala

matatu ya kipaumbele ambayo wangependa Rais ayashughulikie, ikifuatiwa na huduma za afya (asilimia 42). 

Hata hivyo, ripoti hiyo inaeleza kuwa katika miaka ya hivi karibuni, wasiwasi wa umma kuhusu usalama wa chakula uliongezeka zaidi mwaka 2017, ikifuatiwa na umaskini na gharama za maisha kwa ujumla.

“Wasiwasi wa masuala ya kiuchumi umeshuka kidogo mwaka 2021 na 2022 ikilinganishwa na miaka iliyopita, ingawa bado wasiwasi huo juu ikilinganishwa na maswala mengine,” imeeleza ripoti hiyo.

 Wasiwasi kwa huduma za jamii umeongezeka sana mwaka 2021 na 2022 ikilinganishwa na 2020. Hii ipo katika huduma za afya, usafiri, elimu na usambazaji wa maji.

Pia Twaweza katika ripoti hiyo inaeleza kuwa wasiwasi wa masuala ya kiutawala hasa ufisadi na usalama haviko juu sana katika orodha ya vipaumbele vya wananchi.

Follow Us on TikTok

Subscribe to Our YouTube Channel

Subscribe

Loading videos...

Loading videos...

Loading videos...