Idadi ya wabunge wanawake duniani imeongezeka kwa asilimia 0.4
- Rwanda yaongoza kwa kuwa na idadi kubwa ya wanawake wabunge duniani
- IPU yasema ongezeko hilo ni la taratibu sana.
Dar es Salaam. Wakati dunia ikiadhimisha Siku ya Kimataifa ya Wanawake, ripoti ya Umoja wa Mabunge Duniani (IPU) inaonyesha idadi ya wanawake wabunge duniani imeongezeka kwa asilimia 0.4.
IPU ni Shirika la Umoja wa Mabunge lenye wanachama zaidi ya 180 kutoka nchi 193 duniani kote ikiwemo Tanzania ambapo Spika wa Bunge Dk Tulia Ackson akiwa ni Rais wa 31 wa umoja huo.
Ripoti ya IPU iliyotolewa hivi karibuni imeangazia idadi ya wanawake waliochaguliwa bungeni katika nchi wanachama 193 ambapo mpaka kufikia mwishoni mwa mwaka 2023 walikuwa asilimia 26.9 kutoka asilimia 26.5 iliyokuwepo mwaka 2022.
Licha ya ongezeko la asilimia 0.4, IPU imebainisha kuwa idadi hiyo ni ndogo kulinganisha ile iliyorekodiwa mwaka 2020/2021.
“Mwaka 2023, maendeleo ya uwakilishi wa wanawake bungeni yalikuwa ya polepole na mchanganyiko…hii inawakilisha kiwango sawa cha maendeleo kama mwaka 2022, lakini polepole kuliko miaka iliyopita,” imebainisha ripoti ya IPU.
Rwanda kinara kwa idadi ya wabunge wanawake duniani
Kati nchi wanachama 193, Rwanda imefanya vizuri kwa kuwa na idadi kubwa ya wabunge wanawake ikichukua asilimia 61.3 ya viti katika baraza la manaibu katika orodha ya mabunge ya IPU.
Nchi nyingine ni Cuba yenye asilimia 55.7, Nicaragua yenye asilimia 53.9, huku nchi za Andorra, Mexico na Umoja wa Falme za Kiarabu zikiwa na usawa wa asilimia 50.
Mbali na idadi ya wabunge wanawake, IPU imebainisha kuwa idadi ya vijana katika bunge hilo la kimataifa ni asilimia 31.7 ambao wapo chini au umri wa miaka 45.
Idadi hiyo ni sawa na kusema vijana watatu kati ya 10 wameshika nafasi za ubunge katika mataifa mbalimbali duniani.
Kwa takwimu hizo huenda viongozi wa IPU wakawa na jukumu la kuongeza ujumuishi na ushiriki wa wanawake na vijana katika nafasi za uongozi ikiwemo ubunge.