Mwanza yaanza mikakati kuwapanga upya machinga

September 17, 2021 7:22 am · Mariam John
Share
Tweet
Copy Link
  • Manispaa ya Ilemela itatumia wiki mbili kukagua miundmbinu.
  • Wamachinga watapelekwa katika masoko watakayopangiwa.
  • Polisi, migambo kutokuhusika katika zoezi hilo.

Mwanza. Siku chache baada ya Rais Samia Suluhu Hassan kuagiza wafanyabiashara wadogo kupangwa upya, Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela jijini Mwanza imetenga wiki mbili kwa ajili ya kukagua miundombinu katika masoko yote ili yarekebishwe kabla zoezi hilo halijafanyika.

Maagizo ya kuwapanga wafanyabiashara hao maarufu kama machinga pia yalitolewa na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa wakati akizungumza na wakuu wa mikoa Septemba 15 mwaka huu ambapo pia alitoa mwezi mmoja zoezi hilo liwe limekamilika.

Uongozi wa Halmashauri ya Ilemela umeanza kutembelea maeneo yote ya masoko katika eneo lake ili kujiridhisha kama kuna miundombinu yote ikiwemo maji na vyoo.

Ikibainika kuna changamoto za miundombinu, halmashauri utatenga fedha kwa ajili ya kurekebisha.

Mkuu wa Wilaya ya Ilemela, Hassan Masalla amesema toka alipopangiwa kazi katika wilaya hiyo alikutana na changamoto ya wananchi kufanya biashara kwenye maeneo holela.

Amesema Halmashauri hiyo ni manispaa na ni lazima maeneo yake  yapangike vizuri na biashara zifanyike kwa kufuata utaratibu.

Masalla ametaja maeneo makuu ambayo watayatembelea kujiridhisha kama miundombinu yake ipo swa ni pamoja na Kiloleli, Nyasaka, Kirumba, Sabasaba na Buzuruga.

“Inawezekana kuna maeneo aidha tulilegea kidogo au kuna kitu ambacho kimetugharimu hadi tumefika hapa ila hatujachelewa, hivyo masoko tuliyonayo tunataka yaanze kufanya kazi mara moja,” amesema Masalla

Amesema walishawaita viongozi wa machinga ambao nao walikiri kuwa maeneo wanayo walishapewa  ingawa hawajui changamoto ni nini.

Pamoja na zoezi la kuwapanga wafanyabaishara hao pia kitakachofanyika ni kila mfanyabiashara aliyeko barabarani kumjua jina na ikiwezekana apigwe hadi picha kisha zoezi la kuwapanga liendelee mara moja.

“Tumepewa mwezi mmoja, tukiutumia vizuri tunaamini zoezi  litaenda na kuisha kwa amani, tusimame kama timu na tufuate taratibu zote hatutamuumiza mtu na hatutamsukuma mtu kitakachofanyika ni kuwapanga kwa amani,” amesema.

Amesema katika zoezi la kuwapanga machinga halmashauri hiyo haitatumia nguvu na kwamba watafanya kwa ushirikiano ili kila mmoja aende kwenye eneo atakalopangwa.

“Tunataka zoezi hili tulifanye kwa ushirikiano, hatutatumia migambo wala polisi na katika hili halmashauri yetu itakuwa ya mwisho kwenye kutumia nguvu, tumezngumza na viongozi na tunaendelea kuzungumza nao kuona ni changamoto zipi wanazokutana nazo ili sote tusaidizane,” amesema 

Mkuu huyo wa Wilaya amemtaka Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo, Modest Apolinary  kuondoa mfumo wa mrundikano wa uongozi kwenye masoko badala yake uongozi usimamiwe na halmashauri.

“Hii itasaidia katika kuwajua wafanyabaishara hao na hakutakuwa na migogoro ya mara kwa mara,” amesema 

Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Ilemela Angeline Mabula amesema hapo awali zoezi la kuwapanga machinga kwenye maeneo yao lilienda vizuri  na machinga walihamia kwenye maeneo yaliyokuwa yamepangwa.

Anasema hata sasa zoezi hili litafanikiwa kwa kuwa wafanyabiashara hao ni waelewa na wakishirikishwa wataenda bila manung’uniko yoyote.

“Zoezi hili hapo nyuma lilifanyika vizuri ila alitokea mtu mmoja akampigia simu hayati John Magufuli akamwambia wamachinga huku wameteswa wamevunjiwa vitu vyao  ndipo akaagiza wamachinga wote warudishwe kwenye maeneo waliyokuwepo, hivyo niombe viongozi wote tushirikiane kwa pamoja kuhakikisha zoezi hili linaenda na linaisha kwa amani,” amesema Mabula.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW