Machinga waonywa kufanyia biashara maeneo yasiyo rasmi
- Baadhi waanza kuonekana katika ya miji.
- Wadau maeneo waliyopangiwa hayana wateja.
- Serikali kuwachukulia hatua watakaokaidi.
Mwanza. Ikiwa imepita zaidi ya miezi mitano tangu wafanyabiashara wadogo maarufu kama wamachinga kuhamia kwenye maeneo waliyopangiwa na Serikali, baadhi yao wameanza kurudi katika maeneo ya zamai ikiwemo barabarani ili kuendelea na biashara walizokuwa wanafanya.
Nukta Habari (www.nukta.co.tz) imeshuhudia baadhi ya wafanyabiashara katikati ya jiji la Mwanza wakiwa wamezipanga bidhaa zao chini na wengine wakiwa wamezibeba mikononi.
Wafanyabiashara hao wanadai kuwa maeneo mapya waliyopangiwa hayana wateja, jambo linalowalazimisha kurudi katika maeneo yasiyo rasmi.
“Tunaamua kuwafuata wateja kuwapelekea huduma, huko tulikopelekwa wateja hawaji na maeneo yamejaa,” amesema mmoja wa machinga ambaye hakupenda jina lake litajwe.
Serikali iliamua kuwapanga upya wamachinga katika maeneo yanayotambulika ili kupunguza usumbufu kwa watu wengine hasa watumiaji wa barabara.
Soma zaidi:
-
Rais Samia aagiza wamachinga kupangwa upya
-
Wafanyabiashara wasota na soko liloungua miaka saba Dar
- Wafanyabiashara wana la kujifunza kuungua soko la Kariakoo?
Mwenyekiti wa Wafanyabiashara Wadogo mkoani Mwanza, Matondo Masanja amewataka wafanyabiashara kutii agizo la Serikali na kuwa kama uongozi hauko tayari kumsaidia mfanyabiashara ambaye bidhaa zitakamatwa akiwa anafanyia biashara katikati ya jiji.
“Zoezi la kuwaondoa wafanyabiashara lilifanikiwa kwa kiwango kikubwa, maeneo yapo mengi na kuna nafasi za kutosha hivyo niwaombe waende huko mara moja na wasisubiri kusukumwa,” amesema Masanja.
Hata hivyo, Serikali mkoani Mwanza imesema zoezi la kuwahamisha wamachinga lilikamilika a wote walipelekwa katika maeneo yao na hakuna sababu yao wao kurudi tena katika maeneo ya zamani.
Mkuu wa Wilaya ya Ilemela, Hassan Masala amesema wameweka watu wa kuwafuatilia wamachinga watakaoonekana kupanga bidhaa zao kwenye maeneo ambayo hayaruhusiwi na kwamba watakaokamatwa bidhaa zao zitataifishwa na wao kufikishwa mahakamani.
“Tumeweka marufuku ya wamachinga kutofanya biashara katikati ya mji, tunawafuatilia kwa karibu, wale wote wanaokikuka masharti na tukiwakamata tunawafungulia mashtaka,” amesema Masala.
Kauli kama hiyo pia imetolewa na Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana, Amina Makilagi ambaye amewataka machinga kuhakikisha wanaondoka mjini.
Makilagi amesema mpango ulipo sasa ni kuweka mji safi na kupanda miti hususani eneo la Makoroboi ambapo kulikuwa na wamachinga wengi.
Latest
