Wanafunzi 7,364 wapata mikopo elimu ya juu awamu ya pili

October 22, 2021 7:15 am · Mwandishi
Share
Tweet
Copy Link
  • Mikopo hiyo ina thamani ya Sh19.4 bilioni.
  • Inawahusu wanafunzi wa mwaka wa kwanza.
  • Awamu ya tatu kutangazwa Oktoba 25, 2021.

Dar es Salaam. Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) imetangaza orodha ya awamu ya pili yenye wanafunzi 7,364 wa mwaka wa kwanza waliopangiwa mikopo yenye thamani ya Sh19.4 bilioni kwa mwaka wa masomo 2021/22 unaotarajiwa kuanzia wiki ijayo.

Mkurugenzi Mtendaji wa HESLB, Abdul-Razaq Badru katika taarifa yake iliyotolewa leo Oktoba 22, 2021 amesema orodha hiyo iliyotolewa leo inafanya jumla ya wanafunzi wa mwaka wa kwanza waliopangiwa mikopo hadi sasa kufikia 45,095 ayenye thamani ya Sh119.3 bilioni.

Badru amesema kuwa HESLB imeanza kupeleka fedha za wanafunzi waliopangiwa mikopo katika vyuo mbalimbali na kuwataka wanafunzi kupata taarifa za kina katika akaunti walizotumia kuomba mkopo maarufu kama SIPA (Student’s Individual Permanent Account) na kujiandaa kwenda vyuoni kwa ajili ya kujisajili.

“Serikali imeshatupatia fedha na tumeanza kuzipeleka vyuoni … lengo letu ni kuhakikisha wanafunzi wanaopangiwa wanazikuta fedha vyuoni ambako watajisajili na kupokea ili watimize ndoto zao,” amesema Badru.

Amesema HESLB imeshapokea fedha kwa ajili ya malipo kwa wanafunzi waliopangiwa mikopo awamu ya pili  taratibu za malipo  zimekamilika na fedha za wanafunzi zinatarajia kufika vyuoni kuanzia leo Ijumaa, Oktoba 22, 2021.

Kuhusu kutangazwa kwa orodha ya awamu ya Tatu, Badru amesema imepangwa kutolewa Jumatatu, Oktoba 25, 2021 baada ya kukamilisha uchambuzi wa maombi unaoendelea na kuwataka waombaji mikopo kutembelea akaunti zao ya SIPA kupata taarifa kuhusu maombi yao.

“Orodha hii ya pili inajumuisha wanafunzi wenye sifa zikiwemo kuwa wahitaji, wameomba kwa usahihi na wamekamilisha taratibu za udahili wa chuo kimoja … tunakamilisha uchambuzi wa maombi mengine na tutaoa orodha ya tatu katika siku tatu zijazo, yaani Jumatatu Oktoba 25, 2021,” amesema Badru.

Serikali imetenga Sh570 bilioni kwa ajili ya mikopo ya jumla ya wanafunzi 160,000. Kati yao, wanafunzi 70,000 watakuwa ni wanufaika wapya na wanafunzi zaidi ya 90,000 ni wale wanaoendelea na masomo baada ya kufaulu mitihani yao ya mwaka. 

Aidha, Badru amesema HESLB inawasihi waombaji wa mikopo kuwa watulivu wakati mchakato wa upangaji wa mikopo kwa wanafunzi wenye sifa kwa awamu inayofuata ukiendelea.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW