Chanjo ya Uviko-19 inayowafaa watoto
- Ni aina ya Pfizer-BioNTech inayotengenezwa nchini Ujerumani.
- Imethibitishwa kufanya kazi kwa asilimia 90.
- Itasaidia kuepusha maambukizi ya Corona kwa watoto.
Dar es Salaam. Mamlaka ya Chakula na Dawa Marekani (FDA) imeidhinisha chanjo ya Corona (uVIKO-19) aina ya Pfizer-BioNTech kwa watoto wa miaka mitano hadi 11.
Taarifa iliyotolewa na mamlaka hiyo jana imesema chanjo hiyo inayotengenezwa nchini Ujerumani imepitishwa ili kuepusha maambukizi ya ugonjwa huo kwa watoto ambao awali hakukuwa na chanjo kwa ajili yao.
Mathalan, kwa Marekani pekee, asilimia 39 ya visa vya ugonjwa wa Uviko-19 kwa watoto wenye umri chini ya miaka 18 vilitoka katika kundi la watoto wa miaka mitano hadi 11.
Kati ya visa hivyo, watoto 8,300 walifikia hatua ya kulazwa na hadi mwanzoni mwa mwezi Oktoba mwaka huu, watoto 146 nchini humo wameripotiwa kufariki.
Kwa mujibu wa FDA, chanjo hiyo imethibitishwa kuwa na ufanisi wa asilimia 90.7 ya kupambana na virusi vya corona.
“Kuwachanja watoto dhidi ya Corona kunatusogeza karibu na kurejea kwenye hali ya kawaida,” amesema Kaimu Kamishna wa FDA, Dk Janet Woodcock.
FDA imesema chanjo hiyo imekidhi vigezo vyote vinavyotakiwa. tazama video hii fupi kujifunza zaidi.
Makala hii imefadhiliwa na Shirika la maendeleo ya habari la International Media Support (IMS) na Umoja wa Ulaya (EU).

Latest