CCM yampitisha Dk Tulia kugombea uspika
Dar es Salaam. Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya CCM, imepitisha jina pekee la Dk Tulia Akson kuwa mgombea wa kiti cha Spika kati ya wanachama 70 waliokuwa wanawania kuteuliwa na chama hicho kugombea nafasi hiyo.
Dk Ackson ambaye ni Naibu Spika amepitishwa kugombea nafasi hiyo baada ya Spika Job Ndugai kujiuluzu Januari 6, 2022 baada ya kuwepo shinikizo kubwa kutoka kwa watu mbalimbali la kumtaka kujiuzulu kutokana na kauli yake iliyokosoa uamuzi wa Serikali kukopa zaidi mikopo kugharamia miradi ya maendeleo.
Katibu Mwenezi wa CCM, Shaka Hamdu Shaka akizungumza na waandishi wa habari leo Januari 20, 2022 kwenye ukumbi wa White House Dodoma amesema Kamati Kuu imepitisha jina moja la Dk Akson kati ya majina 70 ya makada wa CCM waliochukua na kurejesha fomu.
Kwa muktadha huo, Dk Ackson ambaye ni Mbunge wa Mbeya Mjini atalazimika kujiuzulu nafasi ya naibu spika aliyokuwa anaishikilia tangu mwaka 2015 ili kutoa nafasi kwa mtu mwingine kumrithi.
Kwa mujibu wa Bunge la Tanzania, wabunge wote wanatakiwa kufika Dodoma Januari 31, 2022 kwa ajili ya kuanza Mkutano wa Sita wa Bunge utakaoanza Februari Mosi ambapo moja ya kazi itakuwa kumchagua spika na naibu spika.
“Kwa mujibu wa lbara ya 84 (1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1977, Spika ndiye Kiongozi wa Bunge na ndiye msimamizi wa shughuli zote za Bunge. Aidha, lbara ya 84 (8) inaelekeza kwamba Kiti che Spika kinapokuwa wazi hakuna shughuli yoyote itakayotekelezwa katika Bunge isipokuwa uchaguzi we Spika.” alisema Katibu wa Bunge, Nenelwa Mwihambi Januari 7, 2022.
Latest
