Waziri Mabula: Msijenge nyumba bila vibali

July 15, 2022 12:47 pm · Mariam John
Share
Tweet
Copy Link

Kujenga bila kupimiwa kunasababisha ugomvi na migogoro kati ya mtu na mtu lakini pia ni hatari pale moto unapotokea inakuwa changamoto namna ya kuuzima. Picha| Daudi Mbapani Bunzali.


  • Asema vibali vinasaidia kuanisha maeneo yaliyopimwa.
  • Pia inapunguza migogoro ya ardhi.

Mwanza. Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Dk Angeline Mabula amewataka wananchi kuacha kujenga katika maeneo ambayo hayajapimwa hali inayosababisha miji kutopangika.

Waziri Mabula ametoa angalizo hilo Julai 15, 2022 wakati akizungumza na wazee wa Halmashauri ya Wilaya ya Ilemela ambapo alitumia fursa hiyo kuwakumbusha mabalozi wa mitaa kuwaelimisha wananchi kuacha kujenga bila kuwa na vibali.

Amesema ujenzi usiofuata mipangilio unasababisha miji kuwa skwata haina barabara na kwamba inasababisha kukosa huduma muhimu ikiwemo zahanati, maji na umeme.

“Kujenga bila kupimiwa kunasababisha ugomvi na migogoro kati ya mtu na mtu lakini pia ni hatari pale moto unapotokea inakuwa changamoto namna ya kuuzima,” amesema Dk Mabula.

Waziri Mabula amesema katika halmashauri zote ikiwemo ya Ilemela hivi sasa hakuna mtu anayeruhusiwa kujenga bila kupata kibali cha kujenga.

“Manispaa haina kijiji watu wanajijengea tu mkiwekewa ‘X’ ya kubomolewa mnaanza kupiga kelele kwa mbunge, naomba kupitia nyie wazee tuache kujenga, tuwaambie na majirani zetu huko mlipo asijenge bila kibali hii ni manispaa ipo chini ya mipango miji na hapo tutajikuta tumekaa vizuri,” amesema Dk Mabula.

Mwenyekiti wa Baraza la Wazee Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela, Mohamed Yusuph, amempongeza Waziri kwa kuwambusha wajibu wao kwenye jamii na kwamba suala la kujenga kwenye eneo ambalo halijapimwa sio zuri.

Amesema wameanza kuona madhara hayo ambapo kwa sasa kuna migogoro kati ya jirani na jirani hali inayosababisha kukosekana kwa barabara na endapo ikitokea majanga ya moto mtu atashindwa kupita kwa ajili ya kwenda kuokoa.

“Haya masuala ya kujenga bila kibali yameibuka tu hivi karibuni ambapo zamani enzi za ujamaa hayakuwepo na yalikuwa hayakubaliki licha ya kwamba sheria haikuwepo lakini watu walijenga kwa kufuata taratibu,” amesema Yusuph.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW