Waziri atangaza msamaha wa kodi ya ardhi kwa taasisi za dini
- Msamaha huo ni wa miezi sita tu.
- Watakiwa kulipa madeni sugu bila riba.
Mwanza. Serikali imetangaza masamaha wa kodi kwa wadaiwa sugu wa ardhi zikiwemo taasisi za dini na mashirika kulipa madeni yao bila riba katika kipindi cha miezi sita kuanzia sasa.
Msamaha huo ni kuanzia Julai hadi Disemba mwaka huu ambapo umelenga watu ambao wanadaiwa katika kipindi kisichozidi miaka mitano.
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Angelina Mabula amesema taasisi zinazoongoza kwa kudaiwa madeni ya muda mrefu ni pamoja na taasisi za dini na kuwataka viongozi wa madhehebu hayo kuhakikisha wanatumia fursa ya msamaha huo kulipa.
“Niwaombe wote wenye madeni ya muda mrefu kutumia fursa hii kulipa madeni kwani pamoja na msamaha huo pia Rais Samia Suluhu Hassan ameridhia kupunguza tozo ya asilimia 1 ya kila mwezi ambapo hivi sasa italipwa kwa asilimia 0.5 katika kipindi hicho cha miezi sita na ifikapo mwezi Januari mwakani tozo hiyo itarudi kwenye kiwango chake cha awali,” amesema Mabula.
Mabula alikuwa akizungumza leo Julai 11, 2022 jijini Mwanza kwenye mkutano uliokutanisha pamoja viongozi wa madhehebu mbalimbali ya dini ambao ulilenga kupata uelewa wa Sensa ya watu na Makazi itakayofanyika Agosti mwaka huu.
Soma zaidi:
Waziri Mabula amewataka wenye maeneo yaliyochukuliwa kama ya umma lakini yanasoma majina ya watu binafisi kufanya marekebisho mara moja kwakuwa serikali haitakubaliana kuona migogoro inayotokea baina ya waumini na viongozi wa dini.
Badala yake Serikali itataka kuona viwanja kwa ajili ya kujenga nyumba za ibada viwe na majina ya wadhamini.
Akitolea ufafanuzi wa jambo hilo, Waziri Mabula amesema mathalani dini ya kiislamu italazimika kusajili jina la Bakwata, halikadhalika madhehebu ya kikristo wataandika aidha TEC au wadhamini wengine kulingana na imani zao.
“Tumekuwa na viwanja vingi ambavyo madhehebu yanagongana kwa sababu tu jina la kiwanja linasomeka la mtu binafsi huku kikitambulika kama kiwanja cha dhehebu fulani, kama Serikali hatukubaliani na jambo hilo,” amesema Mabula.
Waziri huyo pia amewataka viongozi hao kuendeleza maeneo ambayo waliomba kwa ajili ya kujenga nyumba za ibada pia kuyaweka katika utaratibu mzuri.
Latest