Twitter isiyo na matangazo mbioni kuzinduliwa
- Ni fursa kwa watu wasiopenda usumbufu wa matangazo.
- Pia itasaidia mtandao huo kuongeza wigo wa vyanzo vyake vya mapato.
- Twitter kuendelea kujivua gamba siku za usoni.
Dar es Salaam. Kama wewe ni miongoni mwa watu ambao hawapendi usumbufu wa matangazo wakati ukitumia mtandao wa Twitter, kuna habari njema kwa ajili yako. Hata hivyo, itabidi ujipange kwa sababu hakuna vya bure.
Mmiliki wa Twitter, Bilionea Elon Musk ameweka wazi mpango wa kuzindua toleo maalum la mtandao huo lisilo na matangazo kwa watumiaji wake watakaoweza kulipia.
Twitter katika taarifa yake ya hivi karibuni imemnukuu Musk akisema “matangazo ya ya Twitter ni ya mara kwa mara na ni makubwa sana. Tunachukua hatua kushughulikia suala hilo wiki zijazo, ” ameongeza kuwa kutakuwa na “usajili wa bei ya juu ambao hauna kabisa matangazo.”
Toleo jipya linalokuja linaangaziwa kuwa na ubora wa hali ya juu na nyongeza za vipengele vipya kuzidi la sasa ikiwemo kumuwezesha mtumiaji kuhariri na alama ya tiki ya bluu ya uthibitisho.
Ikumbukwe kuwa tangu mwishoni mwa mwaka jana Musk alionesha nia ya kutoa toleo lisilo athiriwa na matangazo kabisa kwa watumiaji wake na mchakato huo umekuwa ukiendelea.
“Basic Blue itakuwa na nusu ya idadi ya matangazo. Tutatoa kiwango cha juu bila matangazo mwaka ujao,” Musk aliandika kwenye ukurasa wake wa Twitter Disemba 2022.
Toleo la lisilo na matangazo ni hatua mpya ya mabadiliko makubwa kwa kampuni hiyo kutoka kwenye kutegemea matangazo kama chanzo chake kikuu cha mapato ambayo yamepungua kwa kiasi tangu Musk aliponunua kampuni hiyo Oktoba mwaka jana.
Zinazohusiana:
- Twitter kuwawekea watumiaji wake muonekano mpya
- Facebook kuzuia matangazo ya ‘uponyaji wa miujiza’ mtandaoni
- Maboresho: Kupitia Twitter utatazama video mubashara
Katika Ripoti ya Meneja Mkuu wa Mauzo na Masoko wa Twitter, Chris Riedy alisema wiki iliyopita kuwa mapato ya kila siku yalikuwa chini ya asilimia 40 kutoka siku hiyo hiyo mwaka mmoja uliopita wakati Twitter imekuwa ikipata karibu asilimia 90 ya mapato yake kutokana na matangazo ya kidijitali yaliyowekwa kwenye jukwaa.
Mapema mwezi huu, Twitter pia imelegeza baadhi ya sera zake za muda mrefu zinazopiga marufuku matangazo ya kisiasa kwenye jukwaa la mtandao huo ili kuongeza mapato na kupunguza gharama za uendeshaji.
Twitter inashughulikia pia kipengele kipya cha huduma ya uthibitishaji wa mashirika ya kibiashara. Wanatakaojisajili kwenye huduma hii watapata alama ya dhahabu inayobainisha akaunti kuwa ni ya kibiashara.
Sambamba na hatua hizo ambazo kampuni hiyo inazichukua kuongeza kiwango chake cha mapato, inafanyia kazi mchakato wa kubadilisha pia na sera zake za matumizi ya jukwaa hilo.
Akaunti rasmi ya Usalama wa Twitter ilichapisha Januari 4, 2023 kuwa “Kusonga mbele, tutalinganisha sera yetu ya utangazaji na ile ya TV na vyombo vingine vya habari.’’