Unavyoweza kutalii maeneo mbalimbali duniani kidijitali
- Unahitaji kuwa na intaneti na simu au kompyuta.
- Zitakuwezesha kutalii ukiwa hapohapo ulipo.
Dar es salaam. Ni ukweli usiopingika kuwa tupo kwenye nyakati ambazo matumizi ya teknolojia yamepewa kipaumbele kwa kiasi kikubwa katika kila nyanja ya maisha. Iwe ya kiuchumi, kisiasa au kijamii kama afya na elimu.
Sekta ya utalii nayo haijaachwa nyuma. Hivi sasa hautalazimika tena kufunga safari kutoka sehemu moja kwenda sehemu nyingine ili kutalii bali unaweza kufanya hivyo popote ulipo ikiwa tu una huduma ya intaneti pamoja na kifaa cha mawasiliano kama simu au kompyuta.
Inawezekanaje?
Utalii huu unawezekana kwa kutumia  teknolojia ya uhalisia pepe ambapo video zilizorekodiwa katika maeneo mbalimbali kama miji mikuu, fukwe maarufu, barabara za miji na maeneo ya vivutio huwekwa katika tovuti au programu tumishi  ili kuwafikia watu wengi duniani.
Zifuatazo ni baadhi ya tovuti ambazo unaweza kutumia kutalii sehemu mbalimbali duniani ukiwa hapo ulipo.
Je  unapenda kuendesha gari ukiwa unasikiliza redio huku unafurahia mandhari ya miji tofauti tofauti? Drive&Listen ni tovuti itakayokuwezesha kutimiza hilo.
Kwa kutumia tovuti hiyo utaweza kuendesha magari katika miji tofauti duniani huku ukisikiliza redio zilizopo kwenye mji husika, unaweza kuianza siku yako ukiwa mitaa ya Tokyo nchini Japan na kuimalizia New York, Marekani.
Tovuti hiyo iligunduliwa na  Mhandisi wa Uturuki Erkam Seker na kutambulishwa rasmi mwezi Mei  mwaka 2020.
Upweke uliokuwa unamkabili wakati wa zuio la kutoka nje baada ya wimbi la Uviko-19 ndiyo ulimfanya Seker kubuni njia itakayowawezesha watu duniani kote kuwa na uwezo wa kutembelea miji mingine bila wao kutoka nje.
Tovuti hiyo ina nchi zaidi ya 150 na kupitia tovuti hiyo unaweza kuongeza au kupunguza mwendo wa gari pamoja na kusikiliza sauti halisia za eneo husika kwa wakati huo.
Namna miji inavyoonekana katika tovuti ya Drive&Listen ambapo kuna sehemu pia ya kuchagua mji unaoutaka.Picha | Drive&Listen
Ikiwa wewe ni miongoni mwa watu wanaopenda kufanya matembezi mida ya jioni au asubuhi kwa ajili ya kujionea uzuri wa eneo fulani au kulifahamu zaidi eneo husika basi City Walks ni muafaka wako.
Tovuti hii ilitengenezwa na wahandisi wa programu tumishi akiwemo Aristomenis Georgiopoulos pamoja na Artemis Stiga katika kipindi cha janga la Uviko-19.
Tovuti hiyo imesheheni mandhari  za miji mbalimbali duniani katika nyakati za mchana na usiku ili kukupa muonekano tofauti lakini pia inakuwezesha kusikiliza sauti halisi zilizopo eneo hilo kwa wakati huo.
Soma Zaidi
Window-swap
Je unatamani kufahamu mandhari za miji  mbalimbali kama vile Manchester wa Uingereza  au New Delhi, India inaonekanaje kutokea dirishani? basi tovuti ya window-swap ipo maalumu kwa kazi hiyo.
Tovuti hiyo ilitengenezwa mwaka 2020 na wapenzi ambao ni Sonali Ranjit pamoja na Vaishnav Balasubramanian waliokuwa na lengo la kuwawezesha watu kutizama mandhari za miji au maeneo mengine katika kipindi cha zuio la kutoka nje wakati wa Uviko-19.
Katika tovuti hiyo kuna video kutoka nchi 80 pamoja na zaidi ya video 20,000 za mandhari tofauti ikiwemo miji, bustani, milima na mabonde.
Taswira ya mji wa Oahu nchini Marekani unavyoonekana kutokea dirishani.Pichalwindow swap
Jipange
Teknolojia imethibitisha hakuna kinachoshindikana, ni muhimu kujiandaa kuendana na mabadiliko ya wakati husika ili kutumia vema fursa zitakazoibuka.
Hata hivyo, teknolojia hii inaweza kuwa na changamoto kiasi hasa katika nchi zinazoendelea ambazo upatikanaji wa huduma ya intaneti pamoja na vifaa kama simu au kompyuta ni ghali au siyo wa uhakika.