Ziara ya Rais Samia Ubelgiji yaleta neema Tanzania
Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango na Mlipaji Mkuu wa Serikali, Emmanuel Tutuba, akizungumza wakati wa kikao na ujumbe kutoka Ubelgiji, jijini Dodoma. Kulia ni Balozi wa Tanzania nchini Ubelgiji, Jestas Nyamanga, na kushoto ni Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango, Amina Khamis Shaaban. Picha| Wizara ya Fedha na Mipango.
- Ubelgiji yaahidi kuipatia Tanzania Sh62 bilioni.
- Zitatumika kukuza ujuzi wa ajira kwa vijana wa Kigoma.
- Ziara ya Rais Samia yamia yachangia kupatikana kwa fedha hizo.
Dar es Salaam. Serikali ya Ubelgiji imeahidi kuipatia Tanzania Euro milioni 25 sawa na Sh62 bilioni, kwa ajili ya kutekeleza programu mpya ya maendeleo ya miaka mitano katika sekta ya elimu inakayosaidia kukuza ujuzi wa ajira kwa vijana.
Programu hiyo inayotarajiwa kutekelezwa kuanzia mwaka 2023 hadi mwaka 2027 katika mkoa wa Kigoma.
Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Maendeleo la Ubelgiji (ENABE), Koenrad Goekint ametoa ahadi hiyo Machi 10, 2022 baada ya kukutana na kufanya mazungumzo na Katibu MKuu wa Wizara ya Fedha na Mipango, Emmanuel Tutuba.
Goekint amesema kuwa programu hiyo itajikita katika kuendeleza sekta ya elimu kwa kuangazia maeneo ya ukuzaji ujuzi wa ajira na utaalam kwa vijana hususan masuala ya uanagezi na ujasiriamali.
Itasaidia kuzalisha ajira, kuimarisha usawa wa kijinsia kwa kukuza zaidi ushiriki wa wanawake kwenye shughuli za maendeleo na kuboresha masuala ya usawa wa kijinsia nchini.
Tutuba ameishukuru ENABEL kwa kuja na program hiyo itakayotoa matokeo mazuri kwa kugusa maisha ya wananchi wa Tanzania katika kuwaletea maendeleo.
“Program hii itakayotekelezwa mkoani Kigoma itagusa maeneo ya kipaumbele yaliyoainishwa kwenye utekelezaji wa Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano (2021/22 – 2025/26), wenye lengo la kuboresha huduma za jamii, maisha ya watu na elimu ni moja ya maeneo hayo” amesema Tutuba.
Soma zaidi:
-
Ubelgiji yaipatia Sh11.3 bilioni Serikali ya Tanzania
-
Tanzania itakavyofaidika ziara ya Rais Samia nchini Ufaransa, Ubelgiji
Tutuba ameiomba Serikali ya Ubelgiji kuangalia uwezekano wa kuongeza maeneo mengine ya kimkakati ya kuboresha maisha ya wananchi ikiwemo huduma za afya na maji kwani wanawake ndiyo walengwa wakuu na ndiyo wanaokabiliana na changamoto ya uhaba wa maji.
Ameshauri Serikali ya Ubelgiji kutekeleza mradi kama huo kwa upande wa Zanzibar ili kuwawezesha wananchi wa visiwa hivyo kufurahia matunda mazuri ya uhusiano mwema uliopo kati ya Tanzania na Ubelgiji.
Utoaji wa fedha hizo ni matokeo ya ziara ya Rais Samia Suluhu Hassan aliyofanya kati ya Februari 14 na 19, 2022
Akiwa nchini Ubelgiji, Rais alikutana kwa mazungumzo na viongozi mbalimbali akiwemo Alexander De Croo, Waziri Mkuu wa Ubelgiji ambapo Viongozi hao walikubaliana kuweka mikakati ya kufanyika kwa majadiliano ya programu ya maendeleo na kuhakikisha kuwa mchakato wa maandalizi unakamilishwa kwa wakati.
Tanzania imeingia katika orodha ya nchi 15 pekee duniani ambazo Ubelgiji inaendesha programu kama hiyo, jambo ambalo ni ishara ya mafanikio makubwa ya uhusiano uliopo kati ya nchi hizi mbili.