Zaidi ya Sh2 bilioni kuokoa maisha wanaozama majini Kanda ya Ziwa
- Watu zaidi ya 200 hufariki kwa kuzama majini kila mwaka.
- Wadau kutoa elimu na vifaa kunusuru wavuvi.
Mwanza. Wadau wanakusudia kutumia Sh2.7 bilioni kuokoa maisha ya wananchi wanaoishi pembezoni mwa Ziwa Victoria wakiwemo wavuvi wanaofariki dunia kila mwaka kutokana na ajali za kuzama katika ziwa hilo.
Kwa mujibu wa Shirika la Usimamizi wa Mazingira na Maendeleo la (EMEDO), zaidi ya wavuvi 100,000 wanaofanya shughuli zao na kuishi pembezoni mwa Ziwa Victoria, kati yao 281 hupoteza Maisha kila mwaka kwa kuzama majini.
Mkurugenzi Mtendaji wa EMEDO, Editrudith Lukanga amesema matukio ya ajali za majini yamesahaulika na hakuna jitihada za makusudi kuhakikisha ajali hizo zinapunguzwa.
“Tofauti na ajali za barabarani na zingine zinavyochukuliwa kwa uzito, ajali za majini hazijawahi kupewa kipaumbele hivyo kama shirika tumeona ipo haja ya kuja na mkakati wa kupunguza vifo vya majini kwa kuhakikisha wavuvi wanapoingia ziwani wawe na vifaa vya kujikinga na ajali za majini,” amesema Lukanga.
Kiasi hicho cha fedha cha Sh2.7 bilioni kitatumika katika kutoa elimu ya kujikinga na vifaa kwa wavuvi ili kuwahakikisha wanakua salama wanapofanya shughuli zao ziwani.
Amesema tayari wameanza mkakati wa kupunguza ajali hizo kwa kushirikiana na Serikali kutoa elimu namna ya kujikinga na ajali hizo.
Mkakati huo wa kupunguza ajali majini unatekelezwa na shirika hilo kwa kushirikiana na taasisi kutoka Uingereza inayohusika na masuala ya maji na uokoaji (RNLI) ambao wameingia mkataba wa miaka mitatu kusaidia jamii ya wavuvi.
Ajali za majini husababishwa na matumizi ya vifaa vya duni vya uvuvi, dhuruba na kukosekana kwa elimu ya matumizi sahihi ya maji katika shughuli za uvuvi.
Baadhi ya watu huamini kuwa ajali hizo huchangiwa na imani za kishirikina.
Mratibu wa Mradi wa Kupunguza Ajali za Kuzama Majini kutoka EMEDO, Arthur Mugema amesema ipo haja kwa Serikali kuondoa ushuru kwenye bidhaa za uokoaji majini ili kutoa nafasi kwa wavuvi na wasafiri wa majini kununua bidhaa hizo kwa bei ya kawaida.
Ametaja bidhaa hizo kama makoti ya kuogelea (lifejacket) yanauzwa kwa bei ghali jambo ambalo wavuvi hushindwa kumudu kununua na wakati mwingine hununua ambayo hayana ubora.
“Jaketi yenye ubora na salama huuzwa kati ya Sh40,000 hadi Sh50,000 kiasi ambacho ni kikubwa hasa kwa mvuvi mdogo,” amesema Mugema.