Yaliyojiri bajeti ya Wizara ya Maendeleo na Vijana ikisomwa kwa mara ya kwanza
- Vipaumble, changamoto na mikakati ya kuwainua vijana ni miongoni mwa yalijadiliwa.
Dar es Salaam. Bajeti ya Ofisi ya Rais, Maendeleo ya Vijana imesomwa kwa mara ya kwanza Bungeni Dodoma leo Aprili 20, 2026 tangu kuanzishwa rasmi kwa wizara hiyo na Rais Samia Suluhu Novemba 17 mwaka jana.
Akiwasilisha bajeti hiyo leo Aprili 20, 2026 bungeni jijini Dodoma, Waziri wa Nchi Joel Nanauka ameliomba Bunge liidhinishe Sh35.9 bilioni kwa mwaka wa fedha 2026/27 ili kutekeleza shughuli mbalimbali za wizara hiyo.
Awali masuala ya vijana yalikuwa yakishuguhulikiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Vijana, Ajira na wenye Ulemavu chini ya Waziri Ridhiwani Kikwete
Kwa mujibu wa Rais Samia lengo la kuanzisha wizara hiyo ni kuhakikisha vijana wanapata jukwaa la kusikika na kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya nchi.
Pamoja na kuanzishwa kwa wizara hiyo Rais Samia aliahidi kuanzisha kitengo cha washauri wa vijana ndani ya ofisi ya Rais.
Akizungumza leo Aprili 20, 2026 bungeni jijini Dodoma, Waziri wa Nchi Joel Nanauka, ameeleza kuwa kati ya bajeti hiyo inayosubiri kuidhinishwa na Bunge Sh30.1 bilioni zimetengwa kwa ajili ya matumizi ya kawaida.
Katika kiasi hicho cha matumizi hayo ya kawaida, Sh1.22 bilioni ni kwa ajili ya mishahara, huku Sh28.8 bilioni zikiwa kwa matumizi mengineyo (OC).
Kwa upande mwingine Sh5.85 bilioni zimetengwa kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo, ambapo Sh5 bilioni ni fedha za ndani na Sh853.03 milioni ni fedha za nje.
Aidha, Nanauka amesisitiza ukubwa na umuhimu wa kundi la vijana nchini, akibainisha kuwa zaidi ya vijana milioni 20, sawa na asilimia 34.4 ya Watanzania, wanachangia zaidi ya asilimia 55 ya nguvu kazi ya taifa.
Latest