Wizara ya Afya: kuchangia figo ni bure

September 2, 2025 5:55 pm · Kelvin Makwinya
Share
Tweet
Copy Link
  • Ni ndugu wa karibu pekee ndiye anayeruhusiwa kuchangia figo na mchango huo unafanyika bila malipo yoyote.

Dar es Salaam. Serikali imesema huduma ya kuchangia figo kwa wahitaji wa matibabu hayo ni bure na haifanyiki kibiashara kama ambavyo inaelezwa kwenye taarifa mbalimbali kwenye mitandao ya kijamii.

Taarifa ya Aminiel Aligaesha, Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano na Uhusiano kwa Umma wa Hospitali ya Muhimbili, iliyotolewa leo Septemba 2 ,2025 imeeleza kuwa huduma ya kuchangia figo katika hospitali hiyo inafanywa na ndugu wa mgonjwa husika bila malipo na sio kibiashara.

Kwa mujibu wa Aligaesha Kabla ya mchangiaji kuchangia, kamati ya uidhinishaji inayojumuisha wanasheria, viongozi wa dini, madaktari na maafisa ustawi wa jamii, hupitia maombi ya upandikizaji, kufanya mahojiano na wahusika pamoja na kuthibitisha uhusiano wao kupitia nyaraka muhimu ikiwemo vyeti vya kuzaliwa, viapo, picha na vipimo vya kitabibu.

“Uchangiaji  wa figo unaofanyika nchini Tanzania unasimamiwa na Kanuni za Huduma za Figo za mwaka 2017 zilizopitishwa na Wizara ya Afya kwa kuzingatia miongozo na maazimio ya kimataifa ambayo yanakataza biashara ya viungo vya binadamu,” imeeleza taarifa ya Muhimbili.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, jumla ya wagonjwa 106 wamenufaika na huduma ya kupandikiza figo tangu ilipoanzishwa  Septemba 2017.

Hata hivyo, taarifa hiyo haijafafanua hatua za kisheria zitakazochukuluwa dhidi ya watoa huduma za afya na wananchi watakaoshiriki katika uuzaji au usafirishaji wa kiungo hicho muhimu mwilini kwa mwanadamu.

Muhimbili imesisitiza kuwa itaendelea kutoa huduma hizo kwa kuzingatia kanuni na kufuata viwango vya kimataifa ili kulinda afya na usalama wa wagonjwa pamoja na wachangiaji.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW