Muhimbili yakanusha kuwafuta kazi wafanyakazi 200
- Yasema ililazimika kusitisha mikataba ya muda mfupi kwa wafanyakazi 27 waliokuwa wakihudumu kwa kujitolea baada ya kupata wafanyakazi wapya.
Dar es Salaam. Uongozi wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) umekanusha taarifa zilizosambaa kwenye mitandao ya kijamii zikidai kuwa hospitali hiyo imewafukuza kazi wafanyakazi 200 kutokana na ukosefu wa fedha za kuwalipa mishahara.
Taarifa hizo zilizoenezwa kupitia kurasa za Instagram na Facebook, zilionyesha barua ya mmoja wa wafanyakazi aliyepewa notisi ya kusitishiwa ajira ya mkataba, jambo ambalo uongozi wa Muhimbili umeeleza siyo kweli.
Akitoa ufafanuzi, Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano na Mawasiliano kwa Umma wa Hospitali hiyo, Aminiel Aligaesha, kwenye taarifa yake ameeleza kuwa kwa sasa Muhimbili ina jumla ya wafanyakazi 4,326, ambapo 3,193 wapo Upanga na 1,133 wapo Mloganzila.
“Kati ya hao, wafanyakazi 4,075 wana ajira za kudumu na 251 wana mikataba ya muda mfupi. Ajira za muda mfupi mara nyingi zinahusishwa na miradi mbalimbali ya hospitali, na pindi inapofikia ukomo, mikataba husitishwa kwa mujibu wa taratibu,” imeeleza taarifa hiyo.
Aidha, taarifa hiyo imeeleza kuwa kuanzia Januari hadi Septemba 25, 2025, Muhimbili imepokea jumla ya wafanyakazi 380 wapya wa kudumu, na kutokana na ongezeko hilo, hospitali ililazimika kusitisha mikataba ya muda mfupi kwa wafanyakazi 27 waliokuwa wakihudumu kwa kujitolea ‘volunteers’.
“Hivyo basi, taarifa kuwa hospitali imesitisha ajira za wafanyakazi 200 siyo za kweli. Tunapenda kuwataka wananchi kupuuza taarifa hizo za upotoshaji,” amesisitiza Aligaesha kwenye taarifa yake.
Uongozi wa Muhimbili umesema kuwa utaendelea kuajiri na kusitisha ajira pale inapobidi, kwa kuzingatia sheria, taratibu na kanuni za utumishi wa umma chini ya Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma.