WHO yasikitishwa kasi ndogo ya utoaji chanjo ya Uviko-19 Afrika
- Ni nchi nne zimeweza kufikia kiwango cha asilimia 10 ya wananchi wake wote kupata chanjo.
- Afrika imepata chonjo milioni 87 mpaka sasa
- Ukosefu wa chanjo na utayari wachangia kazi ndogo ya utoaji chanjo.
Dar es Salaam. Huenda ikachukua muda kwa nchi za Afrika kupunguza kasi ya maambukizi ya Corona (Uviko-19) kutokana na changamoto mbalimbali ikiwemo mwenendo usiorodhisha wa utoaji wa chanjo dhidi ya ugonjwa huo unaoutesa dunia kwa sasa.
Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Umoja wa mataifa la Afya UlimwenguNI (WHO) Dk Tedros Ghebreyesus amesema ni nchi nne tu za Afrika ambazo zimeweza kufikia kiwango cha asilimia 10 ya wananchi wake wote kupata chanjo.
“Ulimwenguni, nchi 140 angalau zimechanja wananchi wake kwa asilimia 10, lakini kati ya nchi hizo za kutoka Afrika ni nchi 4 pekee ndio zimeweza kufikia kiwango hicho cha asilimia 10 ya wananchi wake wote, na utofauti huu ni kutokana na kukosa chanjo,” amesema Ghebreyesus.
Dk Ghebreyesus ametoa masikitiko hayo katika mkutano wa kamati ya mawaziri wa afya barani Afrika unaofanyika kwa siku tatu nchini Togo.
Aidha, amesema kuwa usambazaji wa chanjo umekuwa si wa haki kwa kiasi kikubwa kwa sababu ulimwenguni kote chanjo zilizotolewa ni zaidi ya bilioni 4.8 huku Afrika akipata chanjo milioni 87 tu kati ya hizo.
Kiwango hicho cha chanjo ya Uviko-19 kilichofika Afrika ni chini ya asilimia mbili huku akizitaka Serikali na wataalam wa afya kulitazama suala hilo kwa makini ili kuokoa maisha ya watu.
“Hivyo tunatarajia kuona ongezeko la kasi ya utoaji chanjo, mwezi Julai chanjo zimesambazwa kwa kiwango kikubwa ukilinganisha na miezi mitano iliyopita, malengo yetu ni kufikia chanjo milioni 475 ifikapo mwezi Disemba mwaka huu 2021,” Amesema Dk Ghebreyesus.
Pia mkurugenzi wa WHO kanda ya Afrika Dk Matshidiso Moet amesema sektretarieti yake imejipanga vyema kwa miaka ijayo na wanategemea kuimarisha namna ya kukabiliana na Uviko-19 hususan kwenye chanjo ambayo ndiyo itakuwa sehemu muhimu ya kazi yao lakini hii itaenda pamoja na kuimarisha mifumo ya afya.
Latest
