Waziri Kigwangalla: Kazi ya kuzima moto uliozuka Mlima Kilimanjaro ni ngumu
- Amesema kazi ya kuzima moto uliozuka mwishoni mwa wiki ni ngumu na kubwa kuliko inavyodhaniwa.
- Ugumu huo unasababishwa na upepo mkali na kukauka kwa nyasi na vichaka.
- Helikopta na ndege kuanza kutumika kuzima moto huo ikiwa taratibu zitakamilika leo.
Dar es Salaam. Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk Hamisi Kigwangalla amesema kazi ya kuzima moto uliozuka Mlima Kilimanjaro mwishoni mwa wiki ni ngumu na kubwa kuliko inavyodhaniwa kwa sababu ya changamoto ya upepo mkali na kukauka kwa nyasi na vichaka.
Moto huo ulizuka Jumapili Oktoba 11, 2020 katika eneo la Whona ambacho ni kituo cha kupumzikia wageni wanaotumia njia ya Mandara na Horombo kupanda mlima huo mrefu kuliko yote Afrika.
“Bado tunahangaika na kuzima moto. Kazi ni ngumu na kubwa kuliko inavyodhaniwa. Changamoto ni upepo mkali na kukauka kwa nyasi na vichaka,” ameandika Dk Kigwangalla katika ukurasa wake wa Twitter leo (Oktoba 15, 2020).
Amesema kutokana na hali hiyo, wanakusudia kutumia helikopta na ndege kudhibiti moto huo.
“Taratibu zikikamilika leo tutaweza kuanza kutumia helikopta na ndege kuzima moto,” amesema Waziri huyo.
#MzeeWaField kazini Mlimani Kilimanjaro jana. Bado tunahangaika na kuzima moto. Kazi ni ngumu na kubwa kuliko inavyodhaniwa. Changamoto ni upepo mkali na kukauka kwa nyasi na vichaka. Taratibu zikikamilika leo tutaweza kuanza kutumia Helicopters na ndege kuzima moto. #HKpic.twitter.com/PCuRFkUCs1
— Dr. Kigwangalla, H. (@HKigwangalla) October 15, 2020
Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Mawasiliano wa Tanapa, Pascal Shelutete katika taarifa yake iliyotolewa Oktoba 13, 2020 alisema kazi ya helikopta hiyo itakuwa ni kuangalia eneo lililoathirika na kufuatilia maeneo mengine yanayoweza kushika moto.
Amesema jumla ya nguvukazi ya watu 500 wako eneo la tukio kukabiliana na moto huo ambao kwa sehemu kubwa tayari umedhibitiwa.
Soma zaidi:
- Ijue milima 10 mirefu zaidi Tanzania
- Tanapa yaendelea kuchunguza chanzo cha moto Mlima Kilimanjaro
- Moto wazidi kudhibitiwa Mlima Kilimanjaro
Hata hivyo, Tanapa imesema inachukua tahadhari zote ili kuhakikisha usalama wa wageni na vifaa vyao unaimarika bila kuathiri shughuli za utalii ambazo zinaendelea kama kawaida hususan njia ya Marangu iliyoathirika na moto husika.
Mamlaka zinaeleza kuwa wastani wa watu 50,000 hupanda mlima huo kila mwaka.