Wanajeshi wa Pakistan kutoa matibabu bila malipo Dar es Salaam

January 7, 2022 5:19 am · Mwandishi
Share
Tweet
Copy Link
  • Wanajeshi hao wanaweka kambi nchini kama ziara ya ziara ya nia njema.
  • Huduma zitakazotolewa ni pamoja na huduma za madaktari bingwa ikiwemo meno na watoto.
  • Huduma hizo ni bure kwa Watanzania na ‘diaspora’ wa Pakistan.

Dar es Salaam. Watanzania wenye matatizo mbalimbali ya kiafya sasa wamepata fursa ya matibabu baada ya meli ya Wanajeshi wa Pakistan kupiga kambi ya siku mbili jijini Dar es Salaam kutoa huduma za afya bure. 

Ubalozi wa Pakistani nchini Tanzania umeeleza katika taarifa yake iliyotolewa jioni ya Januari 6 mwaka huu kuwa matibabu hayo yatatolewa bure ikiwa ni sehemu ya ziara ya nia njema inayofanywa na Jeshi la Majini la nchi hiyo.

Wataalamu wa afya wa jeshi hilo la Pakistan watatoa huduma hizo za kiafya kuanzia Januari 11 hadi Januari 12, 2022 katika ukumbi wa Diamond Jubilee uliopo Upanga, Dar es Salaam.

Ubalozi huo umeeleza kuwa ujumbe huo wa wataalamu unatarajiwa kuanza kuingia Tanzania Januari 10 kupitia bandari ya Dar es Salaam wakiwa na meli iitwayo PNS ALAMGIR na kutoa huduma za afya bila malipo ndani ya siku hizo mbili. 

“Timu ya Madaktari ya PNS ALAMGIR inafuraha kuwaalika na kutoa huduma hiyo ya matibabu bila malipo kwa watu rafiki wa Tanzania, pamoja na wana ‘Diaspora’ wa Pakistan wanaoishi nchini,” inasomeka sehemu ya taarifa ya Ubalozi wa Pakistan.


Soma zaidi



Kwa mujibu wa taarifa hiyo, timu hiyo itakuwa na wataalamu wa matibabu na ganzi, daktari bingwa wa watoto, daktari bingwa wa upasuaji, daktari wa kinywa na meno pamoja na mpatholojia.

Pia kutakuwa na vifaa vya uchunguzi wa maabara vya magonjwa ya moyo, Ukimwi, uchunguzi wa damu, mkojo, homa ya tumbo pamoja na chumvi.

Huduma nyingine za kiafya zitakazotolewa ni pamoja na uchunguzi wa sukari ya mkojo, kipimo cha figo na kongosho pamoja na kipimo cha kiwango cha mafuta kwenye damu. 

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW