Wagonjwa wa Corona Tanzania wafikia 284

April 22, 2020 10:49 am · Mwandishi
Share
Tweet
Copy Link
  • Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amesema hadi jana 21 Aprili 2020 Tanzania  kulikuwa na watu 284.
  • Idadi hiyo ni ongezeko la wagonjwa 30 ikilinganishwa na 254 walioripotiwa na Waziri wa Afya Ummy Mwalimu Aprili 20 mwaka huu.
  • Watanzania watakiwa kuendelea kuchukua tahadhari ya kujikinga ugonjwa huo. 

Dar es Salaam. Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amesema hadi jana 21 Aprili 2020 Tanzania  kulikuwa na watu 284 waliothibitika kuwa na virusi vya corona huku akiwataka wananchi kuchukua tahadhari wakati wakiendelea na shughuli za kiuchumi na kijamii. 

Idadi hiyo ni ongezeko la wagonjwa 30 ikilinganishwa na 254 walioripotiwa na Waziri wa Afya Ummy Mwalimu Aprili 20 mwaka huu. 

Majaliwa aliyekuwa akizungumza leo (Aprili 22, 2020) katika maombi ya kitaifa ya kuombea nchini dhidi ya COVID-19 jijini Dar es Salaam, amesema kuwa kati ya wagonjwa wote, 256 wanaendelea vizuri kiafya na kupatiwa matibabu na madaktari katika vituo maalum. 

“Jumla ya wagonjwa 284 wamethibitika kuwa na maambukizi ya virusi vya Corona, kati ya hao wagonjwa 256 wanaendelea vizuri kiafya, wagonjwa saba wako kwenye uangalizi wa karibu, kadhalika wagonjwa 11 walishapona kabisa,” amesema Majaliwa.  

Kwa kipindi chote tangu mgonjwa wa kwanza wa COVID-19 ajulikane, Majaliwa amesema watu 10 wameshapoteza maisha.

Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu amesema kati ya wagonjwa wapya 30 waliothibitika jana, 10 wapo Dar es salaam, Zanzibar (9), Mwanza (4), Pwani (2), Kagera (1), Dodoma (2), Manyara (1) na mmoja yupo Morogoro. 


Zinazohusiana


Mpaka sasa jiji la Dar es Salaam ndiyo kitovu cha COVID-19 nchini ikiwa na wagonjwa 143 kati ya wagonjwa 284 walioripotiwa katika mikoa 17ya Tanzania bara. 

Majaliwa amewataka Watanzania kuendelea kuchukua tahadhari ya kujikinga na ugonjwa huo wakati wakiendelea na shughuli zao za kijamii na kiuchumi ikiwemo kuepuka mikusanyiko isiyo ya lazima. 

“Serikali inaendelea kuchukua hatua kadiri itakavyoona inafaa kwa lengo la kudhibiti kuenea zaidi kwa maambukizi ya virusi vya Corona,” amesema Majaliwa. 

Amewataka wananchi waendelee kuiamini Serikali na kuzingatia ushauri na unaotolewa na mamlaka za afya na kuachana na taarifa za upotoshaji zinazotolewa kwenye mitandao ya kijamii. 

Viongozi wa dini nao wametakiwa kutoa elimu ya kujikinga na ugonjwa huo kwa waumini wao hasa wanapokusanyika katika nyumba za ibada. 

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW