Viwanja Afcon vyaongeza bajeti ya michezo mara nane Tanzania
- Bajeti yafikia 285.3 bilioni mwaka wa fedha 2024/25 kutoka Sh35.4 bilioni 2023/24.
- Waziri Ndumbaro asema viwanja vya Dodoma na Arusha vitakamiilka Desemba 2024.
Dar es Salaam. Ujenzi wa viwanja vya mpira wa miguu kwa ajili ya maandalizi ya mashindano ya kombe la mataifa ya Africa (Afcon) umechangia kuongeza bajeti ya Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa mwaka 2024/25 mara nane zaidi ya ile iliyotengwa mwaka jana.
Kwa mujibu wa hotuba ya Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dk Damas Ndumbaro, Serikali imepanga kutumia Sh 285.3 bilioni katika mwaka ujao wa fedha utakaoanza Julai, 2024 kutoka Sh35.4 bilioni iliyoidhinishwa na Bunge mwaka 2023/24.
Kiwango cha bajeti ya michezo kitakachotumika mwaka 2024/25 kingetosha kugharamia shughuli za wizara hiyo kwa miaka minane zaidi iwapo bajeti hiyo ingeendelea kuwa ndani ya wigo wa kiwango kilichopitishwa na Bunge mwaka jana.
Dk Ndumbaro amewaeleza wabunge leo Mei 23, 2024 bungeni jijini Dodoma kuwa asilimia 90 ya fedha hizo zitatumika kutekeleza miradi ya maendeleo ikiwemo ujenzi wa viwanja vya michezo vya Arusha na Dodoma.
“Kati ya hiyo Sh 11.2 bilioni ni kwa ajili ya mishahara, Sh 15.8 kwa ajili ya matumizi ya kawaida na Sh 258.1 ni fedha za miradi ya maendeleo,” amesema Waziri Ndumbaro.
Soma zaidi: Serikali kuinoa timu ya Taifa kuelekea michuano ya AFCON 2027
Aidha, Waziri huyo amewaaambia wabunge kuwa Serikali inaendelea na maandalizi kwa ajili ya michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) ambapo ujenzi wa viwanja viwili vya michezo katika Jiji la Arusha na mkoani Dodoma utakamilika Desemba 2025.
Kwa mujibu wa Waziri Ndumbaro, Serikali imetenga Sh286 bilioni kwa ajili ya ujenzi wa Uwanja wa Mpira wa Miguu mkoani Arusha utakaojengwa na Kampuni ya China Railway Construction Engineering Group Limited (CRCEG) kutoka nchini China.
Mbali na viwanja hivyo Wizara hiyo itaendelea kufanya maboresho ya viwanja vingine ikiwemo uwanja wa Benjamin Mkapa ulipo jijini Dar es Salaam.
Latest