Vijiji zaidi ya 7,000 vyapatiwa umeme Tanzania
- Waziri Mpango amesema Vijiji 7,127 vimeunganishwa na umeme.
- Njia za kusambaza umeme za msongo wa kV 33 zenye urefu wa kilomita 18,227 zimejengwa.
Dar es Salaam. Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Philip Mpango ameliambia Bunge leo jijini Dodoma kuwa uzalishaji wa umeme umeongezaka nchini kutoka GWh 7,092.13 mwaka 2015/2016 hadi GWh 7,374 mwaka 2018/2019 huku vijiji zaidi ya 7,000 vikiwa vimeunganishwa na nishati hiyo.
Dk Mpango amesema ongezeko hilo la uzalishaji wa nishati hiyo limechangia kuongezeka kwa upatikanaji wa umeme wa uhakika.
“Kuongezeka kwa kasi ya usambazaji umeme vijijini hadi kufikia Mei 2019 jumla ya vijiji elfu 7,127 vimeunganishwa umeme ambapo jumla ya taasisi za elimu 3,165, maeneo ya biashara 3,451 pampu za maji 210 taasisi za afya 1,211 na nyumba za ibada 984 zimeunganishwa umeme,” amesema Waziri Mpango wakati akiwasilisha hotuba ya Hali ya Uchumi mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo kwa mwaka 2019/2020.
Hii ni sawa na ongezeko la vijiji 5,109 katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita, ambalo ni ongezeko la asilimia 253 ya vijiji vilivyokuwa na umeme kufikia mwaka 2015.
Zinazohusiana:
- Umemejua unavyoweza kuchangia upatikanaji wa maji safi vijijini
- Maoni: Tunaweza kuwapatia furaha Watanzania wengi kwa nishati jadidifu
- Umemejua kimbilio kwa waliopitwa na gridi ya taifa
Kwa mujibu wa hotuba ya bajeti ya Wizara ya mwaka 2019/2020, ifikapo mwezi Juni, 2020 vijiji zaidi ya10,278 kati ya 12,268 vya Tanzania Bara vitaunganishwa umeme sawa na asilimia 84 ya vijiji vyote.
Dk Mpango amesema mafanikio mengine ni kufikishwa umeme katika vijiji vya wilaya na Halmashauri 15 pamoja na ujenzi wa njia za kusambaza umeme za msongo wa kV 33 zenye urefu wa kilomita 18,227 sambamba na ujenzi wa vituo vidogo vya kupoza na kusambaza umeme 4,100.
Pia ujenzi wa njia ndogo ya usambazaji umeme zenye urefu wa kilomita 30,797.