Mradi wa Sh4.6 bilioni kutoa ahueni ya umeme Lindi, Mtwara
- Wakazi wa maneo hayo sasa wanaweza kuongeza uzalishaji na kuboresha huduma zinazotegemea nishati ya umeme.
Dar es Salaam. Hatimaye ujenzi wa mradi wa laini maalum ya kusambaza umeme kutoka wilayani Masasi hadi Newala umekamilika, hatua itakayosaidia kuimarika kwa upatikanaji wa umeme wa uhakika katika maeneo hayo ya kusini mwa Tanzania.
Mradi huo wa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco), wenye urefu wa kilometa 76, umejengwa na kampuni ya Ujenzi na Ukarabati wa Miundombinu ya Usafirishaji na Usambazaji wa Umeme (ETDCO) na kukamilishwa ndani ya miezi saba.
Sh4.6 bilioni zimetumika katika kugharamia utekelezaji wa mradi huo ambao Waziri wa Nishati, Deogratius Ndejembi amesema ni sehemu ya mkakati wa Serikali kuimarisha upatikanaji wa umeme kusini mwa Tanzania na kuunganisha mikoa ya Mtwara na Lindi kikamilifu na Gridi ya Taifa.
“Serikali imeandandaa mpango mkubwa wa kuifanya Mtwara na Lindi iwe sehemu ya gridi ya Taifa,” amesema Ndejembi
Kwa muda mrefu wakazi wa Lindi na Mtwara wamekuwa wakikabiliwa na changamoto ya kukatika kwa umeme mara kwa mara hali inayokwamisha shughuli mbalimbali ikiwemo uzalishaji.
Kukamilishwa kwa mradi huo wenye msongo wa kilovolti 33 na ETDCO huenda kukaleta ahueni ya upatikanani wa umeme wa uhakika kwa wananchi hao na kuchagiza kuongezeka kwa uzalishaji na uboreshaji wa huduma za kijamii ikiwemo huduma za afya na elimu.
ETDCO ni miongoni mwa kampuni za ndani ya nchi zilizojenga miradi mikubwa ya njia za umeme nchini na miundombinu mingine ya nishati hiyo ndani ya kipindi cha miaka 10.
Kupitia umeme wa gridi ya Taifa sasa wakazi hao wanaweza kufanya shughuli kama kuongeza thamani ya mazao yao ikiwemo kuendesha mashine za kusaga na kukoboa, kuboresha utunzaji wa chakula pamoja na ujasiliamali.
Mkurugenzi Mkuu wa Tanesco, Lazaro Twange, amesema laini hiyo mpya imeongeza uwezo wa mfumo wa usambazaji wa umeme na itasaidia kupunguza kwa kiasi kikubwa adha ya kukatika kwa umeme ambayo wananchi wa Mtwara na Lindi wamekuwa wakiikabili kwa muda mrefu.
Amesema tayari athari chanya zimeanza kuonekana kupitia ongezeko la matumizi ya umeme katika Wilaya ya Newala.
“Kwa wastani Newala ilikuwa inatumia takribani megawati tatu, lakini baada ya kuwasha laini hii matumizi yameongezeka hadi megawati 3.8,” amesema Twange.