Unatumia saa ngapi kufanya kazi kwa wiki?
- Wafanyakazi wanaolipwa na waliojiajiri wenyewe (wenye wafanyakazi na wasio na wafanyakazi) wanatumia muda mwingi kazini ikilinganishwa na makundi mengine.
Dar es Salaam. Licha ya muda wa kufanya kazi kwa watu waliopo kwenye ajira kupungua Tanzania, wafanyakazi wanaolipwa na waliojiajiri wanafanya kazi muda mwingi kuliko makundi mengine.
Kwa mujibu wa ripoti ya Utafiti wa Uwezo wa Kufanya Kazi Tanzania (ILFS) ya mwaka 2020/21 iliyotolewa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) na Ofisi ya Mtakwimu Mkuu wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (OCGS), muda wa kawaida wa kazi umepungua kidogo kutoka wastani wa saa 54 kwa wiki mwaka 2014 hadi saa 53 mwaka 2020/21.
Kupungua kwa muda wa kawaida wa kazi kati ya mwaka 2014 na 2020/21 kumeonekana zaidi kwa wanawake kuliko wanaume. Hali hii inachangiwa na wanawake kutumia muda mwingi katika shughuli za kijamii.
Hata hivyo, masaa ya kufanya kazi yanaendana na viwango vya kimataifa vinavyotolewa na Shirika la Kazi Duniani (ILO) vya kufanya kazi kati ya saa 48 na 56 kwa wiki.
Aidha, matokeo ya utafiti huo yanaonesha kuwa wafanyakazi wanaolipwa na waliojiajiri wenyewe (wenye wafanyakazi na wasio na wafanyakazi) wanatumia muda mwingi kazini ikilinganishwa na makundi mengine.

Saa za kazi ni kipimo cha wastani wa muda ambao watu hutumia kwenye shughuli za uzalishaji wa bidhaa na huduma. Uchambuzi wa muda wa kazi umefanyika kwa kuangalia Saa za Kazi za Kawaida (Usual Hours of Work) na Saa za Kazi za Sasa (Current Hours of Work).