UN yakabiliwa na ukata wa fedha, wafanyakazi hatarini kukosa mishahara
- Shirika hilo liko hatarini kutumia akiba zake zote ifikapo mwishoni mwa Oktoba na kushindwa kuwalipa mishahara wafanyakazi na watoa huduma.
- Katibu Mkuu wa UN, Guaterres amezitaka Serikali zikubaliane juu ya mikakati ya kuhakikisha hali ya kifedha ya Umoja wa Mataifa inakuwa ni nzuri.
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa (UN), Antonio Guterres ameziandikia barua nchi wanachama kuhusu ukata mbaya zaidi kuwahi kukikumba chombo hicho chenye wanachama 193, jambo linalotishia hatma ya mishara ya wafanyakazi na watoa huduma wake.
Akizungumza na waandishi wa habari jana (Oktoba 8, 2019) mjini New York, Marekani, Msemaji wa UN, Stephane Dujarric amenukuu barua hiyo ya Guterres na kusema shirika hilo liko hatarini kutumia akiba zake zote ifikapo mwishoni mwa Oktoba na kushindwa kuwalipa mishahara wafanyakazi na watoa huduma.
Guaterres amezitaka Serikali zishughulikie chanzo cha hali ya sasa ya ukata na zikubaliane juu ya mikakati ya kuhakikisha hali ya kifedha ya Umoja wa Mataifa inakuwa ni nzuri.
Hadi kufikia mwishoni mwa mwezi uliopita, nchi wanachama zilikuwa zimelipa asilimia 70 tu ya fedha kwa ajili ya bajeti ya kawaida ya UN, ikilinganishwa na asilimia 78 katika kipindi kama hicho mwaka jana.
Akisisitiza wajibu wa nchi wanachama kwa mujibu wa Katiba iliyoanzisha UN, Katibu Mkuu ameshukuru nchi zilizolipa michango yao ambazo sasa ni 129 na kusihi zile ambazo hazijalipa kufanya hivyo haraka na kwa ukamilifu.
“hii ndio njia pekee ya kuepusha kutokulipa ambako kunaweza kuathiri operesheni zetu ulimwenguni kote,” amesema Guaterres katika barua hiyo.
Zinazohusiana:
- Prince William atua Tanzania kuendeleza mapambano dhidi ya ujangiri wanyamapori
- Tamasha la ‘Urithi Festival’ kufanyika mikoani kila mwaka
- Mastaa walivyoitangaza Tanzania kimataifa 2018
Hata hivyo amesema tayari sekretarieti anayoongoza ya Umoja wa Mataifa imeshachukua hatua za makusudi kuanzia mwanzoni mwa mwaka huu kuhakikisha kuwa matumizi yake yanaendana na kiwango cha fedha kilichopo.
“Iwapo tusingalichukua hatua za matumizi tangu mwanzoni mwa mwaka huu, pengo la fedha kwa mwezi huu wa Oktoba lingalifikia dola milioni 600 na Umoja wa Mataifa usingalikuwa na uwezo wa kuendesha ufunguzi wa mkutano wa 74 wa Baraza Kuu na vikao vya ngazi ya juu mwezi uliopita.
“Hadi leo hii, tumeweza kuepuka matukio makuu ya kukwamisha operesheni zetu.,” amesema Guterres.
Hata hivyo amesema hatua hizo bado hazitoshi na kuwa Sekretarieti inaweza kushindwa kulipa mishahara na malipo ya bidhaa na huduma ifikapo mwishoni mwa Novemba iwapo nchi wanachama hazitalipa malimbikizo yao yote.
Latest
