TRC yasitisha safari za treni katika mikoa 10

January 31, 2024 5:13 am · Lucy Samson
Share
Tweet
Copy Link
  • Safari hizo zimesitishwa  kutokana na mvua kubwa zinazoendelea kunyesha katika maeneo mbalimbali nchini.
  • Taarifa ya kurejea kwa huduma hiyo itatolewa matengenezo yatakapokamilika.

Dar es Salaam. Huenda watumiaji wa treni jijini Dar es Salaam wakalazimika kutumia njia nyingine za usafiri mara baada ya Shirika la Reli Tanzania (TRC) kusitisha safari za usafiri huo kuelekea katika mikoa 10 ikiwemo Kigoma kutokana na mvua kubwa zinazoendelea kunyesha katika maeneo mbalimbali nchini.

Kwa mujibu wa taarifa ya Jamila Mbarouk, Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano TRC iliyotolewa Januari 30, 2024 safari zilizositishwa ni zile za kutoka Dar es Salaam kuelekea katika mikoa ya Morogoro, Dodoma, Singida, Tabora, Shinyanga, Mwanza, Katavi, Kigoma pamoja na  njia ya kaskazini kuelekea mkoani Tanga.

“Shirika limesitisha huduma kutokana na mvua kubwa zinazoendelea kunyesha maeneo mbalimbali nchini na kusababisha uharibifu wa miundombinu ya reli kati ya stesheni ya Morogoro, Mazimbu…

…Munisagara na Mzaganza Wilaya ya Kilosa mkoani Morogoro, Godegode na Gulwe Wilaya ya Mpwapwa mkoani Dodoma pamoja na eneo la Wami, Ruvu mkoani Pwani na Mkalamo mkoani Tanga,” limesema Shirika hilo.


Soma zaidi: Rais Samia akemea uvuvi haramu Mwanza, aagiza wizara kusambaza nyavu za kisasa kwa wavuvi


Hii inamaanisha kwa watumiaji wa reli kama njia kuu ya usafiri hususan mikoa ya pembezoni kama Kigoma watalazimika kutoboa mifuko yao zaidi ili kugharamia aina nyingine za usafiri kama basi au ndege.

Taarifa ya TRC inakuja wakati Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) ikitoa angalizo la kuwepo kwa hali mbaya ya hewa katiika mikoa nane ikiwemo mkoa wa Morogoro.

Itakumbukwa kuwa kwa majuma kadhaa yaliyopita mkoa huo umerekodi kunyesha kwa mvua kubwa iliyosababisha mafuriko yaliyokata mawasiliano ya njia za usafiri ikiwemo madaraja na barabara.

Aidha, TRC inabainsha kuwa wahandisi kutoka shhirika hilo wanaendelea na matengenezo katika maeneo yaliyoathiriwa na mvua zinazoendelea na taarifa itatolewa mara baada ya kukamilika kwa matengenezo hayo.

Shirika  hilo limeomba  radhi kwa usumbufu uliojitokeza na linawasihi wananchi kuwa wavumilivu katika kipindi cha matengenezo kuhakikisha usafiri unarejea katika hali ya usalama.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW