Tanzania yavunja rekodi ya watalii ya miaka miwili
- Mwaka 2022, watalii milioni 1.45 waliingia Tanzania Bara ambapo idadi hiyo imeongezeka kutoka watalii 922,692 wa mwaka 2021.
Dar es Salaam. Baada ya Serikali kuchukua hatua mbalimbali kukabiliana na janga la Uviko-19, idadi ya watalii imeongezeka kwa asilimia 57.6 ndani ya kipindi cha mwaka mmoja.
Takwimu za Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) zinaeleza kuwa mwaka 2022, watalii milioni 1.45 waliingia Tanzania Bara ambapo idadi hiyo imeongezeka kutoka watalii 922,692 wa mwaka 2021.
Kati ya mwaka 2020 na 2021, Tanzania kama zilivyo nchi zingine duniani, uchumi wake uliathiriwa na janga la Uviko-19. Miongoni mwa athari hizo ni kupungua kwa idadi ya watalii waliokuja kutembelea vivutio vya utalii kutoka na masharti ya ugonjwa huo ikiwemo kuzuia kwa safari za kimataifa na watu kutakiwa kukaa karantini.
Hata hivyo, baada ya kulegezwa kwa masharti ya safari za kimataifa, Tanzania ilianza kuchukua hatua mbalimbali kuimarisha sekta ya utalii ikiwemo kuboresha vituo vya utalii na kuongeza matangazo ikiwemo kutumia filamu ya “Royal Tour” ambayo ilimshirikisha Rais Samia Suluhu Hassan.
Kutokana na hatu hizo, idadi ya watalii wa mwaka 2022 imekuwa ya juu ikilinganishwa na watalii wa mwaka 2020 na 2021.
