Tanzania itakavyookoa mabilioni ujenzi wa kiwanda cha chanjo
Rais Samia Suluhu Hassan akiwa katika ziara yake rasmi nchini Ubelgiji. Picha| Ikulu.
- Ni zaidi ya Sh26.1 bilioni zinazotumika kununua chanjo.
- Pia itaimarisha mapambano dhidi ya Uviko-19.
- Serikali yaanza mipango kujenga kiwanda hicho nchini.
Dar es Salaam. Serikali ya Tanzania imesema hadi kufikia mwaka 2030 itatumia Sh216 bilioni kwa mwaka kwa ajili ya kununua chanjo za magonjwa mbalimbali ikiwemo ya Corona (Uviko-19).
Kiasi hicho cha fedha kitakuwa kimeongezeka kutoka Sh26.1 bilioni iliyokuwa inatumika mwaka 2020 kwa ajili ya kununua chanjo.
Asilimia kubwa ya chanjo hizo huagizwa nje ya nchi kutokana na Tanzania kuwa na viwanda vichache vya kutengeza dawa muhimu za binadamu.
Kwa mujibu wa Wizara ya Afya, katika bajeti ya wizara hiyo kwa mwaka 2021/22 ilitenga Sh63.2 bilioni kwa ajili ya ununuzi na usambazaji wa chanjo katika maeneo mbalimbali nchini.
Huduma za chanjo zilizoboreshwa husaidia kuwakinga watoto chini ya miaka 5, akina mama wajawazito huku chanjo nyingine za kimkakati hutumika kukinga na kudhibiti magonjwa yanayozuilika kama homa ya ini, kichaa cha mbwa na mengineyo.
Pia chanjo hupunguza vifo vya akina mama na watoto wachanga vinavyotokana na uzazi.
Soma zaidi:
-
Kiwanda kinachopambana kuondoa taka mtaani, kuhifadhi mazingira
-
Mwekezaji asota miaka sita kuzindua kiwanda cha nyaya Tanzania
Huenda Tanzania isiendelee kununua chanjo nje ya nchi baada ya Rais Samia Suluhu Hassan kudokeza kuwa Serikali yake inakusudia kujenga kiwanda cha chanjo nchini.
Kiongozi huyo mkuu wa nchi aamewasilisha mpango huo wa Serikali mbele ya Rais wa Baraza la Umoja wa Ulaya (EU) Charles Michael katika akiwa katika ziara ya kiserikali nchini Ubelgiji.
Licha ya kuwa Rais hajasema gharama za mradi huo na sehemu kitakapojengwa kiwanda hicho, lakini kitapunguza gharama za ununuzi wa chanjo kwa Serikali na utaongeza urahisi wa upatikanaji wa chanjo nchini.
Pia kiwanda hicho kitafungua fursa za ajira kwa watalaam wa afya nchini kuendeleza ujuzi wao katika fani ya utabibu.
Kiwanda hicho pia kitakuwa kinatengeneza chanjo ya Uviko-19 ambayo imekuwa ikihitajika katika maeneo mbalimbali duniani.
Tanzania itaungana na nchi nyingine za Afrika ikiwemo Rwanda na Afrika Kusini ambazo zimeanza kujenga viwanda vya chanjo ya ugonjwa huo katika nchi zao.
Novemba mwaka 2021, Rais Samia alipokutana na mwenzake wa Uganda, Yoweri Museveni Ikulu jijini Dar es Salaa alidokeza kuwa nchi hizo mbili zitashirikiana katika ujenzi wa kiwanda cha chanjo.
“Tunataka wataalam wetu wakae wajadiliane tunakwenda vipi kwenye kiwanda hicho,” alisema Rais Samia.