Tamu, chungu waliowekeza soko la hisa Dar
- Wawekezaji wa Kenya Airways watalala na maumivu baada ya thamani ya hisa za kampuni hiyo kushuka kwa asilimia 1.55.
- Wenzao wa Acacia na EABL watalala na tabasabu baada ya thamani ya hisa zao kupanda kwa viwango tofauti.
Dar es Salaam. Wawekezaji wa shirika la ndege la Kenya Airways katika soko la hisa la Dar es Salaam (DSE) leo watamaliza siku kwa maumivu baada ya thamani ya hisa za shirika hilo kushuka na kuwafanya wapoteze Sh5 kwa kila hisa moja.
Hata hivyo, wenzao wa kampuni za Acacia na kampuni ya bia ya Afrika Mashariki (EABL) watalala na tabasamu kwa sababu thamani ya hisa za kampuni zao zimeongezeka kwa viwango tofauti.
Taarifa ya siku ya DSE iliyotolewa leo jioni (Julai 25, 2019) inaeleza kuwa hadi soko linafungwa thamani ya hisa moja ya Kenya Airways ilikuwa ni Sh100 kutoka Sh105 iliyorekodiwa jana.
Wakati wawekezaji wa Kenya Airways wakipoteza Sh5 kwa kila hisa, wenzao wa Acacia leo wanalala na tabasabu baada ya thamani ya hisa za kampuni hiyo kupanda kwa asilimia 1.55 na kuwafanya waweke kibindoni Sh100 kwa kila hisa moja.
Zinazohusiana:
- M-pesa, intaneti vyachangia Vodacom Tanzania kupata faida ya Sh90 bilioni
- Wawekezaji wa Acacia soko la hisa Dar tabasamu tupu
- Maumivu kwa wawekezaji wa kampuni ya bia soko la hisa Dar
Hadi soko linafungwa leo jioni, hisa moja ya Acacia ilikuwa inauzwa Sh6,550 kutoka Sh6,450 iliyorekodiwa jana. Thamani ya hisa za Acacia imepanda kwa siku mbili mfululizo na kuwafanya wawekezaji wa kampuni hiyo ya madini kuendelea kuvuna zaidi.
Barrick Gold, kampuni mama ya Acacia, mwishoni mwa juma lililopita ilifikia makubaliano na Acacia ya kununua asilimia 36 ya hisa ambazo haziimiliki baada ya kuafikiana thamani halisi ya kampuni hiyo yenye migodi ya dhahabu ya North Mara, Bulyanhulu na Buzwagi kuwa ni paundi za Uingereza milioni 951.
EABL nao wana kila sababu ya kutabasamu baada ya thamani ya hisa kampuni hiyo kupanda kwa asilimia 2.37 ambapo hisa moja imeuzwa kwa Sh4,320 kutoka Sh4,220 ya jana.
EABL ndiyo kampuni iliyofanya vizuri zaidi leo sokoni huku nyingi zikibaki katika viwango vilivyokuwepo jana zikiwemo Vodacom, na TICL na kampuni ya habari ya NMG.
Latest
