‘Startups’ 15 za Tanzania kupigwa msasa kufikia viwango vya kimataifa
- Ni programu ya Vodacom Accelerator itakayowasaidia wajasiriamali kuanzisha biashara zenye faida.
- Baadhi ya startups hizo ni pamoja na SmartClass, BongoVocha, na Study Buddy.
- Zitapata mafunzo maalum ya miezi mitatu kutoka kwa wakufunzi waliobobea.
Dar es Salaam. Kampuni ya mawasiliano ya simu ya Vodacom Tanzania imetangaza orodha ya kampuni 15 za wajasiriamali wa teknolojia ikiwemo SmartClass watakaoingia katika awamu ya kwanza ya programu yake ya kidijitali ili kuwajengea uwezo kujiendesha kibiashara na kuwafikia watu wengi.
Programu hiyo iliyopewa jina la “Vodacom Digital Accelerator” ilizinduliwa Septemba 2019 inasimamiwa na Vodacom Tanzania PLC na kituo cha kijamii cha Smart Lab ikiwa na lengo la kuwasaidia wajasiriamali wapya na wanaoendelea kuanzisha biashara zenye faida na zenye kuzalisha kipato.
Taarifa ya Vodacom imezitaja kampuni hizo zinazochipukia (startups) kuwa ni pamoja na BongoVocha, Study Buddy, Food Sasa, MyHi by Innovasie Ltd, Cargo Fleet by Amora, Kasome International, TakaCycle na SmartClass ambayo inawasaidia wanafunzi kusoma mtandaoni wakati huu ambao shule zimefunga.
Startups nyingine zilizofanikiwa kupata fursa hiyo ni NinsiimaeDispensary, Hashtag Pools, Ecoshilling by Hype, Belltro, Wakala Search, Kisomo by Smartcore na Spot ambayo inawezesha upangaji wa matukio mbalimbali mtandaoni.
Kampuni hizo zilizochaguliwa kuingia katika programu hiyo ya mafunzo ya miezi mitatu zinatoka sekta za mawasiliano, teknolojia katika taasisi za kifedha, habari, afya, elimu na biashara ya mtandao (E-commerce).
Kabla ya kuchaguliwa, kampuni hizo zinazochipukia zilipitia hatua mbili ambazo zinajumuisha kutuma maombi na kuchaguliwa na hatua ya mwisho itakuwa kuzisaidia kuongeza kasi ya biashara chini ya wakufunzi mahiri wa teknolojia na ujasiriamali.
Soma zaidi:
- Ni historia: watumiaji wa intaneti tanzania sasa wafikia milioni 23
- Vodacom, Mastercard zaangazia biashara ya mtandaoni kupitia Virtual Card
- Window 95 yaja kivingine baada kutoweka sokoni kwa miaka 18
Vodacom imeeleza kuwa kampuni hizo pia zitawezeshwa kuongeza wigo wao wa kuwafikia wawekezaji, wabia, teknolojia ya kisasa na mtandao wa kibiashara.
“Teknolojia ya dijitali haibadilishi namna tunavyofanya biashara Afrika bali pia inabadilisha tunavyotazama na kutatua masuala yanayohusu maendeleo.
“Kwa hiyo ni kwa heshima kubwa kwamba tutatengeneza fursa ya kutambua fikra kama hizo, kuziunga mkono na kuziboresha kwa lengo la kukuza manufaa yake katika jamii,” alisema Mkurugenzi Mtendaji wa Vodacom Tanzania, Hisham Hendi wakati wa uzinduzi wa programu hiyo.
Baada ya mafunzo ya vitendo kwa miezi mitatu, startups hizo zitapata fursa nyingine ya kuwasilisha mawazo yao mbele ya wawekezaji ambapo tatu kati yao zitachaguliwa kusonga mbele zaidi.
Startups hizo tatu zitapata mafunzo maalum ya miezi sita yatakayojumuisha masuala ya masoko, uwekezaji na kuijua vizuri mifumo ya Vodacom ambayo watafanya nayo kazi.
Programu hiyo inakusudia kuifikisha Tanzania katika ulimwengu wa kidijitali na kuhamasisha fikra za biashara katika sekta ya teknolojia ambazo zitaleta mabadiliko endelevu.
We are excited for the next 3 months and equally look forward to innovative products ranging in Fintech, Media, Agriculture, Health, e-commerce, and Telecommunication at the end of the program, therefore, we all look forward to generating the next Africa’s startup success story. pic.twitter.com/4lgaoPhK2T
— Edwin (@iEdwn) May 6, 2020
Latest