Ahueni, maumivu: Startups za Tanzania wakati wa Uviko-19
- Asilimia 70 ya startups zinapata changamoto ya kujiendesha baada kupungua kwa mapato
- Startups 3 kati ya 10 zimeimarika wakati wa janga la Uviko-19.
- Wadau washauri kupunguza kodi na kuanzisha mfuko wa kuzisaidia startups ili usaidie kutunisha mitaji yao.
Dar es salaam. Tangu kuanza kwa janga la Uviko-19 nchini Tanzania, utendaji wa kampuni zinazochipukia (Startups) umeathirika kutokana na changamoto na athari za ugonjwa huo huku baadhi zikishindwa kabisa kufanya shughuli zake.
Ripoti ya Chama cha Kampuni zinazochipukia Tanzania (TSA) kuhusu athari za Uviko-19 ya mwaka 2020, inaonyesha kuwa asilimia 65 au ya startups za Tanzania mapato yake yalipungua kwa zaidi ya asilimia 50. Hii ina maani kuwa startups mbili kwa kila tatu zilizopo Tanzania zilipoteza nusu ya mapato yake kutokana na Uviko-19, jambo lililorudisha nyuma safari ya ukuaji wa kampuni hizo na kupunguza mchango wao katika ukuaji wa uchumi.
Vilevile, asilimia 2.5 ya startups zinazojihusisha na uingizaji na usafirishaji bidhaa nje ya nchi zilishindwa kufanya shughuli zake kutokana na vikwazo vya usafiri kukabiliana na Uviko-19. Maoema mwaka jana baada ya Uviko-19 kuingia katika mataifa mbalimbali ulimwenguni mipaka ilifungwa kiasi cha kuathiri zaidi sekta ya usafirishaji na utalii.
Licha ya changamoto hizo, ripoti hiyo iliyotolewa hivi karibuni inaonesha kuwa “startups” 3 kati ya 10 zimeimarika huku asilimia 30 ya kampuni hizo zikipata ongezeko la mapato katikati ya janga la uviko-19.
