Stamico yapunguza utegemezi kwa Serikali
- Umepungua hadi kufikia asilimia 9.2 mwaka wa fedha wa 2022/23.
- Ni baada ya kuongeza vyanzo vya mapato.
Mwanza. Shirika la Madini la Taifa (Stamico) limepunguza utegemezi kutoka Serikalini ili lijiendeshe kwa fedha zake ambapo utegemezi hadi kufikia asilimia 9.2 mwaka wa fedha wa 2022/23.
Kiwango hicho kimepungua kutoka asilimia 89 mwaka 2018/19.
Mkurugenzi wa Sera na Mipango wa Wizara ya Madini Augustine Ollal ameeleza hayo wakati akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa maazimio kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kwenye kikao kilichofanyika Bungeni jijini Dodoma.
Ollal amesema Stamico imeweza kuanzisha miradi yake kutokana na fursa mbalimbali zinazojitokeza ili kuongeza vyanzo vya mapato ya ndani na kupunguza utegemezi serikalini ili shirika lijiendeshe kibiashara.
Ollal amesema mapato ya shirika yameongezeka kutoka Sh5.86 bilioni kwa mwaka wa fedha 2019/20 hadi Sh48.5 bilioni mwaka 2012/22.
Mkurugenzi Mtendaji wa Stamico, Dk Vanance Mwasse amesema baada ya changamoto ya kupanda kwa bei ya nishati ya mafuta, shirika limeangalia namna bora ya kulipa deni lake ambapo mpaka sasa shirika limelipa zaidi ya Sh1.7 bilionina linategemea kuanza kulipa Sh600 milioni kila mwezi mpaka deni litakapomalizika.
Mbunge wa Jimbo la Nyasa Stella Manyanya amesema, Serikali iangalie namna ya kulisaidia shirika kulipa mkopo wa Sh18.7 bilioni ili wadai mbalimbali wapate haki zao na kufanya biashara zao baada ya kulidai shirika hilo kwa muda mrefu.
Pia, Mbunge wa Jimbo la Ulanga Salim Hashim ameitaka Serikali kuangalia namna ya kuziongezea halmashauri mapato yatokanayo na sekta ya madini ambapo amesema tozo zitokanazo na mrabaha ambayo ni asilimia 7 ipunguzwe kwa asilimia 2 ili asilimia 5 iende Serikali Kuu na asilimia 2 ibaki kwenye halmashauri husika.
Naibu Waziri wa Madini Dk Steven Kiruswa ameishukuru kamati hiyo kwa maagizo iliyoyatoa na kuahidi kuyafanyia kazi maagizo hayo yenye lengo la kuiboresha sekta ya madini.
“Wizara ya Madini tutaendelea kufanyia kazi maelekezo na ushauri wa Kamati ili kuhakikisha Sekta ya Madini inakuwa na hatimaye kufikia mchango wa asilimia 10 kwenye Pato la Taifa ifikapo mwaka 2025,” amesema.
Wizara ya Madini imetoa taarifa ya utekelezaji wa maazimio yaliyowasilishwa na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kwa kipindi cha Februari 2022.
Latest
