Serikali ya Tanzania yapendekeza kuwalipa posho watendaji wa kata, tarafa
- Madiwani wao wataanza kupatiwa posho zao kwenye akaunti ili kuwaondolea usumbufu na kuongeza ufanisi kazini.
Mwanza. Serikali inapendekeza kuanza kuwalipa madiwani posho zao kwenye akaunti zao kuanzia mwaka wa fedha 2021/22 ili kuondoa usumbufu unaojitokeza na kuongeza ufanisi katika shughuli zao za kila siku.
Waziri wa Fedha na Mipango, Mwingulu Nchemba ameliambia Bunge jijini Dodoma leo Juni 10 kuwa kilio cha madiwani hao kimesikika na wamekuwa wakifanya kazi kwa wakati mgumu kiasi cha kuwakosesha ufanisi kazini.
Amesema kilio cha viongozi hao wa Serikali za mitaa kimesikiwa na sasa Serikali kuu imependekeza kuanzia mwaka wa fedha 2021/22 madiwani hao wataanza kulipwa posho zao kupitia kwenye akaunti zao.
Katika maboresho hayo ya posho, Dk Nchemba aliyekuwa akisoma makadirio ya mapato na matumizi kwa mwaka wa fedha 2021/22, amesema kuwa maofisa tarafa nao watapatiwa posho ya Sh100,000 kwa mwezi.
Waziri Nchemba amesema kumekuwepo na kilio cha maofisa tarafa kukosa posho kwa ajili ya kununulia mafuta kwenye pikipiki zao na kueleza kuwa kuwa kilio hiki kimesikiwa.
“Serikali inapendekeza kuanzia mwaka 2021/22, kuanza kulipa posho ya madaraka ya Sh100,000 kwa mwezi kwa kila Mtendaji Kata kupitia mapato ya ndani ya halmashauri yaliyokuwa yakitumika kulipa madiwani,” amesema.
Latest