Simu mpya za Android kuzipiku iPhone kwa ubora?
- Ni baada ya Android kuingiza sokoni chipu mpya uendeshaji simu.
- Chipu hiyo inatajwa kuwa na kasi na ufanisi mkubwa kuliko simu za iPhone.
Dar es Salaam. Huenda umekuwa ukichukulia poa matumizi ya simu zitumiazo mfumo wa endeshi wa Android, lakini kwa siku chache zijazo huenda simu zake zitakuwa na ufanisi mkubwa kuliko simu mpya za iPhone 14.
Shirika la uundaji programu na huduma za teknolojia la Qualcomm la Marekani linatarajiwa kufanya mkutano wake kati ya Novemba 15 na17, 2022 ili kuzindua chipu mpya ya Snapdragon 8 Gen 2 inayotarajiwa kuzidi ubora wa utendaji na kasi ya chipu zinazotimiwa sasa na kampuni ya Apple.
Taarifa iliyochapichishwa kupitia mtandao wa androidcentral inatoa maelezo kuhusu chipu mpya ya Snapdragon 8 Gen 2, ikisema kwamba “tunaweza kuona toleo la “masafa ya juu zaidi” la chipu mpya mwaka wa 2023.”
Inaonekana, chipu hii inaweza kufikia kasi ya masafa ya 3.4-3.5GHz. Kwa kulinganisha, hii itakuwa juu kidogo kuliko Snapdragon 8+ Gen 1 inayotumika kwenye baadhi ya simu bora zaidi za Android leo, zikitumia masafa ya 3.2GHz.
Chapisho hilo pia linapendekeza kuwa chipu mpya inaweza kupokea ongezeko la kitengo cha usindikaji wa picha (GPU) na kwamba nguvu ya ajabu ya GPU ya chipu hiyo inaweza kushinda nguvu ya chipu mpya ya A16 Bionic kutoka Apple.
soma pia
Kumbuka kwamba utendaji mahiri wa simu unategemea mambo mengi, siyo tu kasi ghafi ya chipu inayoendesha kila kitu. Ufanisi wa usimbaji wa programu, kiasi cha RAM inayopatikana na usimamizi wa halijoto ya simu.
Tofauti na mfumo wa Android, Apple inasimamia mchakato wake mzima wa ubunifu wa programu zenye kasi na maunzi (hardware) zinazotumika kwenye simu zake, bila kutegemea watengeneza chipu wengine.
Mabadiliko hayo mapya yatashuhudiwa mapema kwenye simu za Samsung Galaxy S22, Samsung Galaxy Z Fold 4, Xiaomi 12 Pro, OnePlus 10 Pro, Sony Xperia 1 IV na zaidi zinazotumia Snapdragon 8 Gen 1.
Latest
