Simbachawene: Zaidi ya asilimia 40 ya watumishi wa umma Tanzania hawafanyi kazi
- Ni kwa mujibu wa utafiti uliofanywa hivi karibuni na Tume ya Utumishi wa Umma Tanzania.
Dar es Salaam. Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora George Simbachawene amesema zaidi ya asilimia 40 ya watumishi wa umma nchini hawafanyi kazi licha ya kulipwa mshahara kila mwezi.
Simbachawene amesema hiyo ni kwa mujibu wa utafiti uliofanywa hivi karibuni na Tume ya Utumishi wa Umma Tanzania.
Waziri Simbachawene aliyekuwa akifunga Kikao kazi cha tano cha Serikali Mtandao leo Februali 14, 2025 jijini Arusha amesema watendaji wakuu wa taasisi za umma wana wajibu wa kuhakikisha kila mtumishi anatekeleza majukumu yake ipasavyo.
‘’Watumishi ni lazima wafanye kazi kwani wasipofanya kazi wanakuangusha wewe mkuu wa taasisi, lazima tuwe na jamii inayoandaliwa kufanya kazi’’ amesisitiza Simbachawene.
![](https://i0.wp.com/nukta.co.tz/wp-content/uploads/2025/02/2.jpeg?resize=1024%2C683&ssl=1)
Sehemu ya washiriki wa kikao kazi cha tano cha Serikali Mtandao kilichofanyika kwa muda wa siku tatu jijini Arusha ambacho kimefungwa leo na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora George Simbachawene. Picha l Lusungu Helela
Simbachawene ameongeza kuwa, kwa mujibu wa tafiti hiyo, wavivu, wazembe, wagonjwa pamoja na waliosusiwa kutokana na vipaji na uwezo wao ni asilimia 40 ya watumishi wanaolipwa pasipo kufanya kazi
Hata hivyo, amewataka wakuu hao wa taasisi kuwatumia watumishi wa umma wenye vipaji na uwezo badala ya kuwafanyia fitina na hujuma hali inayosababisha kurudisha nyuma maendeleo ya nchi.
“Kumeibuka tabia ya baadhi ya watendaji wakuu pindi mtumishi mwenye sifa za ziada anapohamia kwenye taasisi anayoiongoza hupata hofu na kutompangia majukumu kwa hisia kuwa ametumwa kumchunguza au kuchukua nafasi yake,
Tabia hiyo kwenye utumishi wa umma haikubaliki na wale wenye tabia hiyo wajirekebishe haraka ,Taasisi hizo ni za umma na sio mali yao binafsi,” amesema Simbachawene.
Katika hatua nyingine, kutokana na ongezeko la matumizi ya simu kwa wananchi, Simbachawene amezitaka taasisi za umma kutoa huduma za kidijitali kutokana na fursa hiyo huku akitoa onyo kwa taasisi ambazo hazijaanza kutumia mfumo wa kidijitali wa e-Mrejesho kuanza kuutumia mfumo huo mara moja kabla ya kuchukuliwa hatua za kisheria.
Latest
![](https://i0.wp.com/nukta.co.tz/wp-content/uploads/2025/02/download-3-1024x696-1.jpeg?fit=300%2C204&ssl=1)
![](https://i0.wp.com/nukta.co.tz/wp-content/uploads/2025/02/VFLt5vHV7aCoLrLGjP9Qwm.jpg?fit=300%2C169&ssl=1)
![](https://i0.wp.com/nukta.co.tz/wp-content/uploads/2025/02/images-96.jpeg?fit=300%2C157&ssl=1)
![](https://i0.wp.com/nukta.co.tz/wp-content/uploads/2025/02/Gi21YlZXgAAxQ2l.jpg?fit=300%2C200&ssl=1)