Serikali yatoa kauli Watanzania waliopo Sudan, yalaani mapigano

April 19, 2023 11:43 am · admin
Share
Tweet
Copy Link
  • Serikali yasema Watanzania takriban 210 waliopo nchini hawajaathirika na mapigano.
  • Mipango ya kuwarudisha nyumbani inaendelea.
  • Tanzania yalaani mapigano hayo ikizitaka pande zinazohasimiana kumaliza tofauti zao kwa njia ya mazungumzo. 

Dar es Salaam. Serikali imesema kuwa hakuna Mtanzania aliyeathiriwa na mapigano yanayoendelea nchini Sudan na inaandaa mpango wa kuwachukua kadiri inakavyohitajika, huku akizitaka pande zote mbili zinazohusika kutumia njia za amani kumaliza mgogoro huo. 

Kauli hii ya Serikali inakuja zikiwa zimepita siku nne tangu yazuke mapigano kati ya vikosi vya Jeshi la Sudani na Vikosi vya msaada ambapo mpaka sasa watu takriban 200  wameripotiwa kupoteza maisha huku wengine zaidi ya 1,000 wakijeruhiwa

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Dk Stergomena Tax aliyekuwa akitoa msimamo wa Serikali kuhusiana na hali inayoendelea nchini Sudan leo Aprili 19, 2023  amewaambia wabunge kuwa nchini Sudan kuna Watanzania wapato 210 ambao wako salama.

“Tunao Watanzania takriban 210 nchini Sudan, kati yao 171 ni wanafunzi na wengine ni maafisa wa ubalozi na raia wengine. Hadi sasa hakuna Mtanzania aliyeripotiwa kuathiriwa na mapigano hayo,” amesema Dk Tax.

Tax amesisitiza kuwa Serikali ya Tanzania inaendelea na juhudi za kuhakikisha Watanzania na raia wengine waliopo nchini humo wanakuwa salama huku mipango ya kuwarejesha nyumbani ikiandaliwa.

“Serikali inaendelea kufuatilia na kuandaa mpango wa kuwachukua Watanzania (evacuation) kadiri itakavyohitajika,” amesema Tax jijini Dodoma


Soma zaidi:


Tanzania yatoa pole, yalaani mapigano

Pamoja na kutoa pole kwa raia wa Sudan na wale wote walioathirika na mapigano hayo, Tax amebainisha kuwa Serikali ya Tanzania inalaani mapigano hayo ya kugombea madaraka huku ikizitaka pande zote mbili kumaliza tofauti zao kwa njia ya mazungumzo.

Kwa mujibu wa Dk Tax, Tanzania ikiwa kama mjumbe wa Baraza la Usalama la Umoja wa Afrika (AU) imeungana na mataifa mengine barani Afrika pamoja na Umoja wa Mataifa (UN) kulaani mapigano hayo na kushawishi kupatikana kwa suluhu kwa njia ya amani.

Mapigano baina ya vikosi viwili vya kijeshi vinavyoongozwa na majenerali Abdel Fattah al-Burhan, ambaye ni  kiongozi wa Kikosi cha Wanajeshi wa Sudan (SAF) pamoja na Mohamed Hamdan Dagalo, wa Kikosi cha Dharura (RSF) yamesitishwa kwa muda wa saa 24 kuanzia jana saa 10:00 jioni ili kupisha misaada ya kiutu baada ya pande mbili hizo kukubaliana.

Taifa la Sudan halijawa katika hali ya utulivu wa kisiasa tangu yalipofanyika mapinduzi ya kijeshi yaliyomuondoa madarakani aliyekuwa Rais wa taifa hilo Omar Al-Bashir mwaka 2019.

Kwa muda sasa wananchi wa taifa hilo la kaskazini mwa Afrika wamekuwa wakishinikiza uongozi wa jeshi kuachia madaraka kwa uongozi wa kiraia jambo ambalo limekuwa likipigwa kalenda na viongozi hao wa kijeshi mpaka yalipotokea mapigano Aprili 15 mwaka huu. 

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW