Serikali yatoa tahadhari homa ya manjano
- Ugonjwa huo umelipotiwa nchini Kenya.
- Yawataka wananchi kuchukua tahadhari ugonjwa huo usiingie nchini.
- Yaimarisha upimaji mipakani na hospitali kuzuia maambukizi.
Dar es Salaam. Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu amewatahadharisha Watanzania kuchukua hatua dhidi ya ugonjwa wa Homa ya manjano ambao umeripotiwa kuwepo nchini Kenya ikiwemo kupata chanjo dhidi ya ugonjwa huo.
Ummy katika taarifa yake iliyotolewa leo Machi 9, 2022, amesema Serikali imepokea taarifa kutoka Shirika la Afya Duniania (WHO) ya kuwepo kwa mlipuko wa ugonjwa huo nchini Kenya ambao unaweza kuingia nchini.
Kwa mujibu wa Ummy, ugonjwa huo tayari umegharimu maisha ya watu watatu huku watu 15 wakiwa na maambukizi nchini Kenya.
Kutokana na hali hiyo, amewataka Watanzania kuchukua hatua ya kuhakikisha ugonjwa huo hauingii Tanzania kwa sababu mpaka sasa hakuna viashiria vyovyote kuwa ugonjwa huo upo nchini.
“Hapa nchini taarifa ya kipindi cha miezi mitatu iliyopita katika mfumo wa ufuatiliaji wa magonjwa zinaonyesha kuwa hakuna taarifa zinazoashiria kuwepo kwa ugonjwa wa homa ya manjano, pia taarifa za ufuatiliaji wa tetesi za magonjwa haujaashiria kuwepo kwa ugonjwa huo,” amesema.
Hatua ambayo inachukuliwa na Serikali kwa sasa ni kuboresha mifumo ya kutoa vyeti vya kielektroniki vya homa ya manjano mipakani ili kuzuia udanganyifu unaoweza kusababisha kusambaa kwa maambukizi.
“Tutaboresha mifumo ya kutoa vyeti vya kielektroniki vya homa ya manjano mipakani ili kuzuia udanganyifu unaoweza kufanywa na maafisa kuwapa vyeti watu ambao hawajachoma chanjo,” amesema Waziri Mwalimu.
Pamoja na tahadhari hiyo, Waziri Mwalimu ameziagiza hospitali zote za rufaa nchini kuwa na huduma za kupima na kutoa chanjo ya homa ya manjano kwa wasafiri na wenye uhitaji.
Soma zaidi:
- Simulizi ya mwanamke aliyejifungua katikati ya mashambulizi Ukraine
- Mashaka ya maumbile yanavyozuia penzi la kweli
- Ukosefu wa nishati safi unavyorudisha nyuma maendeleo ya wanawake Mkuranga
Pia amewaagiza maafisa wa afya mipakani kuhakikisha wasafiri wanaoingia kutoka nchi zenye maambukizi wanakua na vyeti vya chanjo dhidi ya ugonjwa huo.
Dalili za ugonjwa wa homa ya manjano kama homa, kuumwa kichwa, maumivu ya misuli na mgongo, mwili kutetemeka, kupoteza hamu ya kula, kichefuchefu na kutapika.
Dalili nyngine ni pamoja na mwili kuwa wa njano pamoja na kutokwa na damu sehemu za wazi.
Latest